Kurasa

HARAKATI ZA MARAFIKI WA ELIMU NI NINI?

HARAKATI ZA MARAFIKI WA ELIMU NI NINI?
Ni harakati za watu wanaojali na wenye nia ya kuleta mabadiliko katika kuboresha elimu na demokrasia nchini. Harakati hizi zinawaleta pamoja wananchi wanaopenda maendeleo ya elimu na zinawapa fursa ya kubadilishana mawazo na uzoefu katika masuala yanayohusu elimu .Sera na mipango mbalimbali ikiwemo mpango wa maendeleo ya elimu ya msingi (MMEM) na mpango wa maendeleo ya elimu ya sekondari (MMES) inasisitiza ushiriki wa wananchi katika utekelezaji wake.Hivyo wananchi wote wanawajibu wa kuchangia uboreshaji wa elimu na demokrasia nchini. kujiunga na harakati hizi za marafiki wa elimu ni bure na hakuna malipo yoyote wasiliana nasi kwa namba 0755 65 00 75 au 0786 65 00 75 au e-mail jmrchrd@yahoo.com tukuunganishe na marafiki wa elimu popote ulipo Tanzania

Alhamisi, 19 Desemba 2013

Waziri wa elimu adai yeye si waziri mzigo




Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa, ameamua kuvunja ukimya na kueleza kuwa yeye si waziri mzigo na wala hashtushwi na jina hilo kwani hawezi kuzuia maamuzi ya watu kumuita hivyo.

Dk. Kawambwa amesema yeye ni mchapakazi na tayari juhudi za kiutendaji katika wizara anayoiongoza zimeanza kuonekana.

Amesema kuwa suala la kuitwa waziri mzigo linatokana na yeye kuwa kioo na dira ya wenzake  katika wizara hiyo na hivyo majina kama hayo hayawezi kukwepeka na wala kuathiri utendaji wake na kujivunia kuwa yeye ni mmoja wa wasimamizi wa upatikanaji bora wa elimu hapa nchini.

 Waziri Kawamba aliamua kuvunja ukimya huo wakati akifungua kikao cha kazi cha maofisa elimu wa mikoa na halmashauri kinachojadili maendeleo ya elimu ya msingi hapa nchini pamoja na kufanya udahili wa pamoja katika matokeo ya darasa la saba.

"Kuna mtikisiko mkubwa katika wizara yetu na mengi yanasemwa wote mnasikia na Watanzania wanafahamu. Tupo katika safari nzito lakini ili gari liondoke, lazima kwanza litikisike, hivyo msiwe na wasiwasi tutafika salama tu," alisema Dk. Kawambwa.

Alisema anashangazwa kuitwa mzigo kwani kutokana na uwajibikaji wake katika wizara hiyo kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa elimu, wamepata mafanikio makubwa hususani katika kuinua kiwango cha ufaulu wa wanafunzi mtihani wa taifa wa kuhitimu elimu ya msingi mwaka 2013.

 Alisema kutokana na jitihada zake na kushirikiana na watendaji na wadau mbalimbali, kiwango cha ufaulu mwaka 2013 kwa wahitimu wa elimu hiyo ya msingi

kimeongezeka kutoka asilimia 31 mwaka uliopita hadi kufikia asilimia 50.61 mwaka 2013 ambao ufaulu huo ni ongezeko la asilimia 19.89 ukilinganishwa na mwaka jana.

Waziri Kawambwa alisema jumla ya watahiniwa 844,938 walifanya mtihani wa kuhitimu elimu ya msingi na kati yao 427,606 sawa na asilimia 50.61, wamefaulu kwa zaidi ya alama 100 kati ya 250 matokeo ambayo aliyaita ni mazuri.

Alisema kuwa kati ya watahiniwa hao waliofaulu, wasichana ni 208,227 sawa na asilimia 46.68 na wavulana ni 219,379 sawa na asilimia 55.01kitu ambacho kimeinua kiwango cha ufaulu.

Hata hivyo, alisema ufaulu huo bado haujafikiwa lengo la mpango wa Matokeo Makubwa Sasa la kufikia asilimia 60, lakini kutokana na jitihada na kipindi kifupi tangu mpango huo utangazwe, ni wazi kuwa kazi imefanyika na kustahili kupongezwa.