Kurasa

HARAKATI ZA MARAFIKI WA ELIMU NI NINI?

HARAKATI ZA MARAFIKI WA ELIMU NI NINI?
Ni harakati za watu wanaojali na wenye nia ya kuleta mabadiliko katika kuboresha elimu na demokrasia nchini. Harakati hizi zinawaleta pamoja wananchi wanaopenda maendeleo ya elimu na zinawapa fursa ya kubadilishana mawazo na uzoefu katika masuala yanayohusu elimu .Sera na mipango mbalimbali ikiwemo mpango wa maendeleo ya elimu ya msingi (MMEM) na mpango wa maendeleo ya elimu ya sekondari (MMES) inasisitiza ushiriki wa wananchi katika utekelezaji wake.Hivyo wananchi wote wanawajibu wa kuchangia uboreshaji wa elimu na demokrasia nchini. kujiunga na harakati hizi za marafiki wa elimu ni bure na hakuna malipo yoyote wasiliana nasi kwa namba 0755 65 00 75 au 0786 65 00 75 au e-mail jmrchrd@yahoo.com tukuunganishe na marafiki wa elimu popote ulipo Tanzania

Jumanne, 17 Juni 2014

Hali ya Elimu Tanzania

moja ya darasa shule ya msingi Bisumwa wilaya ya butiama


nchi haiwezi kuendelea na watu wachache wanaopata fursa za kipekee kwenye shule chache huku elimu ya jamii pana ikiwa mashakani. Hakuna haja ya kulumbana wala kuingiza siasa katika elimu, bali serikali itekeleze mipango na sera zilizopo na kuboresha mapungufu kwa kushirikisha wadau, na ukweli wa hali ya elimu nchini usisulubiwe wala kubezwa bali tuupokee na kuuwekea mikakati kwa pamoja tuweze kuboresha elimu yetu. pa kuanzia ni kila mmoja katika eneo lake,na kikubwa kufanya zaidi ya mazoea

Jumatano, 11 Juni 2014

changamoto ya elimu toka Geita


Walimu 97 katika shule ya msingi Nyankumbu na Mkombozi katika Wilaya ya Geita, wanatumia tundu moja la choo ambacho kipo kwenye nyumba ya mwalimu huku wanafunzi wa shule hizo 3,563 wakitumia matundu 14 ya choo na kuhofiwa kutokea magonjwa ya milipuko.

chanzo. jamii forums

Jumanne, 10 Juni 2014

kelele za Mbatia kuhusu ubora wa elimu je anasikilizwa?

james mbatia
Mbunge James Mbatia unajisumbua. Natambua uchungu ulio nao juu ya kudorora kwa sekta ya elimu, na natambua uhitaji wako wa mabadiliko katika sekta hii mapema inavyowezekana, lakini unajisumbua.

Sisemi kuwa ukate tamaa, na mimi sikati tamaa, ila naona unazungumza na watu ambao hawawezi kuelewa maana ya kile unachosema na kuhimiza. Nataka nieleza yafuatayo.

Mwaka jana ulipozungumza kuhusu mitaala, kuwa hakuna na kuwa sekta ya elimu inaendeshwa mzobemzobe kama Waluguru ambavyo wangesema, na kuwa vitabu vinavyotumika katika shule zetu havina uhakika wa ubora wake walikubeza, walikutukana, walikutenga, na kukuona mzushi.

Lakini wiki mbili baada ya kuahirishwa kwa Bunge, matokeo ya mitihani yakatoka, na kilichotokea, kuhusu kufeli kwa wanafunzi, Mungu tu anajua.
Mungu alikulipia na kuwaaibisha wale waliodhani kuwa ulikuwa mzushi, na ukarabati uliofanyika kuhusiana na matokeo hayo, na unaondelea kufanyika, sijui, ni suala la kuliombea taifa liondokane na pepo huyu ambaye hataki sisi tulioko serikalini tusikilize mawazo ya wananchi wenzetu.

Kuwa wananchi wenzetu wanapotushauri wanaonekana kuwa ni adui, na kuwa lengo lao sio kujenga ufanisi katika kutoa huduma bali kwa waliotupigia kura, bali kwa sababu wanataka kutujengea hoja tushidwe uchaguzi ujao.

Mbatia, unapokuwa na serikali ambayo wasiwasi wake ni kama itashindwa uchaguzi wa miaka mitano ijayo, na sio kama miaka mitano ijayo watakuwa na cha kuwaonyesha wananchi, katika orodha ndefu ya ahadi ndani na nje ya ilani ya uchaguzi waliyoinadi, sidhani kama unachokisema kitaeleweka.

Tumeona mwaka 2011, mara baada ya uchaguzi malumbano yakaanza ndani ya wanaserikali na walioko nje ya serikali, lakini wote wa chama kimoja, wakifanya maandalizi ya uchaguzi wa 2015.

Vikundi vya uchaguzi wa 2010 havikuvunjwa, kwa kweli vikaimarishwa na kampeni za uchaguzi kiaina zikaanza kwa makini kabisa, hadi walipoonyana wenyewe kwa wenyewe, lakini wale wenye masikio magumu wanaendelea bila kujali kitu.

Sasa hawa watu unapowaambia kuhusu kuimarisha sekta ya elimu unadhani inawezekana kweli, mawazo sio katika huduma bali katika kufanikisha chaguzi.

Mbunge Mbatia, maendeleo kwa wananchi kwa sasa, wewe unajua, sio kigezo cha kuchaguliwa. Hizo siasa zako ni za kizamani.

Sasa hivi unachaguliwa kwa sababu unaweza kutoa takrima, unaweza kuwanunulia watu ubwabwa wakashiba, ukawanunulia watu t-shirts, kofia na khanga, na kuwaimbisha nyimbo jioni wakala wakashiba.

Wananchi wa siku hizi hawaoni uhakiki wa utendaji wa walio madarakani kama ni kigezo, bali uwezo wake wa kutoa rushwa kwa wapiga kura. Sasa unapokuwa na uhakika wa kushinda kwa kutumia fedha na sio utendaji, unaanzaje kufikiria kuboresha elimu.

Elimu haikuwa kwenye ajenda wakati wa uchaguzi, ilitamkwa majukwaani kwa sababu mdomo haukosi cha kuzungumza ukikaa mbele ya kinasa sauti.

Kitu kingine ambacho unanishangaza James Mbatia ni kuwa huoni dunia inakwendaje?. Fasheni siku hizi ni kuhakikisha kuwa  watoto wanakwenda kusoma nje, na kama ni ndani basi katika shule za watu wakubwa, na wewe ukiwemo, nitashangaa kama haumo, kuwapeleka watoto kwenye English Medium, au sijui International Schools.

Unashangaa, mimi hapa ni waziri wa elimu, ofisa elimu, mkurugenzi wa elimu, mwalimu wa sekondari au mwalimu wa shule ya msingi, nimepewa dhamana ya kuhakikisha kuwa elimu inaboreshwa, na tulidhani kigezo kimojawapo ni kutuona sisi wenyewe tunawasomesha watoto wetu nje au ndani, lakini katika shule za serikali.

Lakini aka! Sasa kama tuliopewa dhamana ya kuboresha elimu tunakwepa shule zetu wenyewe, si ujue kuwa kuna jambo ambalo ni bovu tunaliona, na hatusemi ila tunawahamisha watoto wetu. Watoto wa masikini wajua wapi pa kuwapeleka wa kwao.

Kumeundwa kampeni kuwa wazazi wawagharimie watoto wao, badala ya kuimarisha shule za serikali, wanahimiza kuanzisha shule za binafsi.
Hivi kama kweli serikali ina nia ya kuboresha elimu, hao wazazi ambao wanalipa mabilioni ya fedha kwa ajili ya watoto wao, kama wangelipa robo tu ya hizo fedha kwenye shule za serikali kama ada, na serikali ikaweza kuboresha huduma na ubora wa, elimu, kungekuwa kweli na malalamiko dhidi ya sekta ya elimu?

Tungewaokoa wazazi wangapi ambao wanalipa ada kwenye shule ambazo hazina chochote ila utapeli. Lakini nadhani hatuwezi kufikiria kwa umakini.
Tunataka majibu rahisi kwa kitu kigumu, na hatutaki kufikiria kwa mkakati—strategically, bali kwa kuishi kama tulivyozoea.

Mbatia, tunahitaji kupungwa pepo huyu ambaye hataki kusikiliza vilio vya Watanzania kuhusu elimu.

Ijumaa, 6 Juni 2014

Kenya wanafunzi wanaenda na laptop shuleni Tanzania wanaenda na vidumu vya maji na fagio.

waziri mkuu Mizengo Pinda
Mbunge Maryam Salum Msabaha (Viti Maalum, Chadema), ameitaka serikali kutoa maelezo kuhusu chenji ya rada iliyotolewa ili kusaidia kupunguza tatizo la madawati katika shule za nchini kwa kuwa mpaka sasa wanafunzi wanaendelea kukaa sakafuni huku nchi jirani ya Kenya wanafunzi wake wakienda la Laptop.

Msabaha aliuliza katika kipindi cha maswali na majibu ya papo hapo ambayo hujibiwa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, kila Alhamisi.

Alisema nchi yoyote iliyoendelea duniani ilianza kuwekeza kwenye elimu na kutoa mfano wa nchi ya Malyasia, lakini hapa nchini watoto wanabeba madumu ya maji na fagio na kuketi sakafuni, wakati nchi jirani ya Kenya wanaenda na Laptop shuleni.

“Tuliambiwa chenji ya rada itapunguza tatizo mashuleni, lakini mpaka sasa watoto wanakaa chini na dawati moja wanakaa watoto mpaka watano,” alisema.

Akijibu, Waziri Mkuu  Pinda alisema jitihada ambazo serikali inafanya kuhusu elimu ni kuchukua maamuzi makubwa ambayo yamefanya suala la elimu kuzaa changamato kubwa kutokana na uandikishaji wa darasa la kwanza hadi la saba kuongezeka na kusababisha mahitaji  ya shule za sekondari, elimu ya juu ya vyuo vikuu kuongezeka.

Aliwataka Wabunge waendelee kusaidia serikali  ili bajeti ya Wizara ya Elimu iendelee kukua siku hadi siku kwani kukua kwa bajeti hiyo kutaongeza mambo mengi.

Katika swali  la nyongeza Msabaha alitaka kujua wakati huu wa utandawazi wa Sayansi na Teknolojia, serikali inachukua hatua gani kuona wanafunzi wa shule za msingi wanaanza kwenda shule na Laptop.

Hata hivyo, wakati akijibu, Waziri Mkuu Pinda alimhoji “unataka laptop kwa watoto wote wa shule inawezekana? Kwa sababu lazima uulize hilo swali.”

Alisema suala la wanafunzi wa darasa la kwanza mpaka la saba si kuwa na Laptop bali ni kuwa na mfumo wa digitali ambao utamwezesha vitabu vyake vyote kuwa ndani ya kompyuta kwa kutumia kifaa kinachoitwa tablets  badala ya kubeba mzigo mkubwa wa vitabu.

Jumanne, 3 Juni 2014

wanafunzi DIT wagoma kufanya mitihani

Wanafunzi wa Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT) wamegoma kufanya mitihani ya muhula kutokana na wenzao 684 kutopatiwa namba za mitihani kwa madai ya kutokamilisha usajili.

Mgomo huo umesababisha mitihani iliyopangwa kufanyika jana asubuhi na mchana kutofanyika kutokana na wanafunzi hao kugomea kuingia vyumba vya mitihani.

Akizungumza na NIPASHE Rais wa serikali ya wanafunzi, Himida Elihuruma, alisema wamelazimika kugomea mitihani hiyo kwa sababu kuna wanafunzi walifanya usajili tangu Februari, lakini hawajapewa namba za mtihani kwa maelezo kuwa hawajakamilisha taratibu.

“Kuna wanafunzi wamesajiliwa baada ya kukamilisha taratibu zote tangu Februari, lakini  la kusikitisha hawajapatiwa namba kwa kuambiwa kwamba hawajafanya usajili,” alisema Elihuruma.

“Ofisi ya Uhasibu imegubikwa na rushwa, kuna ushahidi wa baadhi ya viongozi na wanafunzi waliombwa ili watafutiwe fomu ambazo zimepotea hali iliyopelekea hadi leo kutopata namba za mtihani,” alisema.

Aidha, alisema kumekuwapo na ubaguzi unaofanywa na utawala kwa kuwanyima namba za mitihani wanafunzi waliokamilisha usajili na kuwapa ambao hawajakamilisha. Aliongeza kuwa uongozi wa chuo umekuwa na utaratibu mbovu wa kupanga tarehe za usajili na kwa mara ya kwanza ilipangwa Machi 7  ikasogezwa Mei 16 hadi 23, mwaka huu bila kutoa taarifa kwa wanafunzi.

Wanafunzi waliohojiwa na gazeti hili walisema hawatafanya mitihani hiyo hadi pale wenzao watakapopewa namba.

Ofisa Uhusiano wa taasisi hiyo, Amani Kakana, alisema mgomo huo hautambuliki na mitihani iliyogomewa jana itapangwa tena na usajili hautaongezewa muda.

“Tulitoa muda wa kutosha wanafunzi kufanya usajili walioshindwa kufanya kwa wakati hawawezi kupatiwa namba, tunafuata utaratibu wa chuo uliopangwa unaoleweka na wanafunzi,” alisema Kakana.

“Mwanafunzi anayejielewa hawezi kugomea mtihani, ratiba haitaharibika itaendelea kama ilivyopangwa, tutamchukulia hatua kali mtu yeyote atakayejaribu kuchochea vitendo vya uvunjifu wa amani,” alisema.

souce ippmedia & nipashe

Jumapili, 1 Juni 2014

Matukio ya elimu katika Picha

TAFAKARI CHUKUA  HATUA YA KULETA MABADILIKO YA ELIMU NCHINI KILA MTOTO APATE ELIMU SAWA ISIYO NA UBAGUZI.


Elimu iwakumbushe vijana faida na hasara za ukoloni ( na Mtemi Gervas Zombwe)

Hoja yangu tangu wiki iliyopita ni kuwakumbusha vijana kufahamu vyema historia yao hasa kuhusu ukoloni na athari zake, ili wajipange vyema kutumia fursa zilizopo na kuendeleza jamii zao.
Nilisema kuwa baada tu ya mkutano wa Berlin uliofanyika Ujerumani mwaka 1885, bara lote la Afrika liliwekwa chini ya utawala wa matapeli wastaarabu, wanaojulikana kama Wazungu kutoka Ulaya.
Mtemi Zombwe
Sababu za kuja kwao na kukalia maeneo yetu, akili zetu, na utamaduni wetu zilidhihirika pale walipoanzisha mifumo yao ya uzalishaji na ukusanyaji wa mapato na malighafi.
Nilitaja baadhi ya athari za ukoloni kuwa ni pamoja na mauaji makubwa, unyanyasaji, kupora utajiri wa Afrika, kugeuza Waafrika kuwa vibarua wa dezo, ukatili, dhuluma, kuvuruga akili za Waafrika na kuua mifumo ya viwanda na teknolojia iliyokuwa imeshamiri katika jamii zetu.
Mbinu walizotumia kufanikisha utii na kuvuruga akili za Waafrika ni kupandikiza dini za kigeni na mafundisho mchanganyiko, huku wakinyang’anya ardhi za Waafrika, kuwaua ama kuwatesa.
Waliendelea kuwapa utumwa wa kiakili na mitazamo duni ili washindwe kufikiri vizuri. Wakawahimiza wawapende maadui zao (ambao ni wao wazungu), wakawahimiza wasamehe saba mara sabini(ili usihesabu viboko ulivyopigwa jana ukiwa uchi).
Waafrika wakaambiwa mila zao ni za kishetani (ili wafuate mila za wazungu wawatawale kirahisi). Na wakacholewa sanamu ya shetani mweusi inayotisha sana. Lakini malaika-wazungu, mitume-wazungu, watakatifu-wote wazungu.
Waafrika wakaogopa! wakaacha mila zao njema wakabeba mzigo wa mila za kishenzi zilizopakwa manukato ya kila aina ili zinukie na zivutie. Hizi ndizo zinazowatesa dada zetu kutamani uzungu kwa kuchubua ngozi zao, kudharau asili yao na hata uumbwaji wao.
Kila cha mzungu ni chema hata kama ni kinyesi na kila cha Mwafrika ni kibaya. Hili likamomonyoa maadili ambayo hadi leo tunayajutia. Wao kicheko!
Hata wasomi wakipelekwa Ulaya kwenda kupata maarifa, hawarudi na maarifa. Wanarudi na utamaduni wa kizungu, ufisadi wa kizungu, dharau za kizungu na ulevi wa kizungu. Maarifa wanayaacha huko huko. Wanarudi vichwa vyeupe vimejaa uzungu-na tamaa ya utajiri pasipo kufanyakazi.
Ndiyo maana kwa sasa tuna utawala wa kizungu, mienendo ya kizungu, lugha za kizungu, dini za kizungu, miujiza ya kizungu, nguo za kizungu, vyombo vya kizungu, na magonjwa ya kizungu.
Pia utamaduni wa kizungu, nyimbo za kizungu, viboko vya kizungu, dawa za kizungu, ufisadi wa kizungu, rushwa ya kizungu, taabu za kizungu, umasikini wa kizungu, Mungu wa kizungu na manabii wa kizungu, matusi ya kizungu, hata uzinzi wa kizungu. Hizi ndizo tunu za ukoloni tulizoachiwa.
Yaliyo mema ya Waafrika yakapotea, yakadharauliwa, yakabezwa na mizigo ya laana ikavijaza vichwa vya Waafrika hao wachache waliokwenda sambamba na mdundo wa mafunzo ya wazungu. Babu zetu wengi walipinga; lakini mwenye nguvu mpishe.
Siyo kila kitu waliachofanya wakoloni ni kibaya kwa Waafrika. La hasha! Yako mambo mengine mazuri kuigwa kwa kuoainisha na mahitaji yetu.
Kwa mfano, jitihada ya kufikiri, kubuni na kufanyakazi kwa bidii ni jambo jema linaloweza kuigwa. Ona kwa sababu ya shida walizopata, walithubutu kuondoka kwao maelfu ya kilomita kuja Afrika ambako hawakukuta pamba wala dhahabu zilizokuwa tayari. Bali wakikuta misitu mikubwa mapori ya kutisha wanyama wengi na udongo wenye rutuba.
Tena mapori mengi Waafrika waliyatumia kama kivuli katika shughuli za unyago. Na misitu mingine ilitumiwa kama sehemu za ibada na matambiko ya jadi.
Lakini wao wakakata nyasi na miti.Wakabuni mashamba na uchimbaji wa madini yaliyokuwa chini ya ardhi, ambayo hata Waafrika wenyewe hatukuyajua kama yapo. Wakathubutu kuchimba na kulima, wakafanikiwa.
Hilo likawezekana wakazoa utajiri mkubwa wakapekeka kwao. Bado huko huko kwao hawakuiacha pamba sebuleni, bali wakabuni mitindo mbali mbali ya usokotaji wa nyuzi ambazo zilikuja kutumiwa kuunda nguo za kila aina zilizouzwa kwao, Asia, Amerika na pia kwetu Afrika.
Mpira uliolimwa Congo wakabuni matairi ya magari wakapata pesa. Shaba waliichukua kwa wingi pale Zambia na Kongo wakabuni nyaya za umeme wakafanikisha umeme ukawaka Waafrika tukafurahia. Je, bila kufikri haya yangewezekana?
Hata wanasayansi wengi waliogundua kanuni na fomula nyingi zilizotumika kutengenezea vitu kama magari, ndege hawakuwa na vyeti vingi, bali kufikiri, kuthubutu na kubuni ndiyo siri ya mafanikio. Walitumia muda wao mwingi kufikiri na kubuni kikamilifu hadi wakaibuka na manufaa hayo makubwa yaliyoibadili dunia hii.
Kina Isaac Newton, Charles Darwin, Plato,Faraday, Garileo, James Watt, Abbot Lambert na wengine wengi ni mifano ya wafikirivu wakubwa ulimwenguni. Je, hawa walikuwa na digrii ngapi hadi wakaweza kufikiri?
Wakati sisi tunaiga uzungu badala ya maarifa na ubunifu, wenzetu Wachina na Wahindi wanaiga maarifa na ubunifu. Wachina wanachukua karatasi wanapaka rangi, wanabuni aina za mikunjo na kukunja karatasi linakuwa ua.
Wanaleta kwetu kama maua ya gharama sana. Tunanunua! Tembelea kwenye masoko duniani kote, bidhaa za Wachina zimetawala masoko, kutokana na kazi za wabunifu na watu wanaothamini kazi na kufikiri.

chanzo. mwananchi

vituko vya elimu kutoka Ruangwa, Lindi

Walimu wa kike wa shule za msingi wilayani Ruangwa mkoani Lindi, wanaogopa kutoa adhabu kwa wanafunzi wa kike kutokana na wanafunzi hao kuwachukulia waume zao kama kulipiza kisasi kwa adhabu wanayopewa na walimu wao.

Kadhalika walimu wa kiume wanaogopa kutoa adhabu kwa wanafunzi wakiume kwa hofu ya kuchomewa nyumba zao moto.

Mwalimu wa kike ambaye hakupenda jina lake liandikwe gazetini alisema aliwahi kutoa adhabu kwa mwanafunzi wa darasa la tano ambaye alimchukulia mumewe wa ndoa ili kumkomesha.

Alisema alimuonya mwanafunzi huyo bila mafanikio na kuamua kwenda kwa Afisa wa Ustawi wa Jamii ambaye alisaidia kunusuru ndoa yake.
Alisema kutokana na hali hiyo walimu wote wa kike wanaogopa kutoa adhabu kwa wanafunzi wa kike.

Utafiti wa kihabari uliofanywa na Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (Tamwa), kuhusu ukatili, unyanyasaji wa kijinsia kwa wanawake na watoto, katika Wilaya ya Ruangwa mkoa wa Lindi, umebaini kuwepo kwa hali hiyo.
Chama hicho kinafanya utafiti wa kihabari katika wilaya kumi za Tanzania Bara na Zanzibar.

Akiongea na NIPASHE, Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Mkata kata ya Nandagala, Wilaya ya Ruangwa, Ismail Chikandanda, alisema kuna uadui mkubwa kati ya walimu na wazazi kutokana na kutokupenda watoto wao kupewa adhabu.

Chikandanda, alisema katika tukio moja wanafunzi walipigana, mwalimu alimchapa mtoto aliyeanzisha ugomvi lakini baada ya kipindi mwanafunzi alitoka darasani na kwenda kumuita bibi yake ambaye aliita wanakijiji wakiwa na silaha kumtafuta mwalimu aliyemwadhibu mwanafunzi huyo.

Mwalimu wa kiume ambaye hakutaka jina lake liandikwe gazetini alisema nyumba ilichomwa moto na wanakijiji baada ya kumwadhibu mwanafunzi wa kiume.

Mwalimu Mkuu msaidizi wa shule ya Msingi Ruangwa, Sharifa Hassan, alisema kuwa tatizo kubwa linalowafanya wanafunzi kuwa na tabia mbaya ni kutokana na ngoma za jando na unyago wanazochezwa na kujiona wako sawa na wakubwa.

Afisa Elimu Kilimo na Ufugaji wa Wilaya ya Ruangwa Yussuf Chilumba, alisema tatizo kubwa ni wazazi kutokuwa na mwamko wa elimu, kwani hata wazazi wao hawakusoma hali inayowafanya kushindwa kusimamia maendeleo yao ya elimu,
“Wazazi wanawaomba wanafunzi wao wasifanye mtihani vizuri ili wasifaulu kwani watawapa shida ya kuwasomesha,” alisema Diwani wa kata ya Nandagala, Wilaya ya Ruangwa, Adrew Chikongwe, alisema kuwa ugomvi kati ya wazazi na walimu ameumaliza na kuanzia wakati huu kutakuwa na amani na hali ya elimu itaendelea vizuri ikiwa ni pamoja na kuwahimiza walimu kuwafundisha kwa bidii watoto.

chanzo.Ipp media