Kurasa

HARAKATI ZA MARAFIKI WA ELIMU NI NINI?

HARAKATI ZA MARAFIKI WA ELIMU NI NINI?
Ni harakati za watu wanaojali na wenye nia ya kuleta mabadiliko katika kuboresha elimu na demokrasia nchini. Harakati hizi zinawaleta pamoja wananchi wanaopenda maendeleo ya elimu na zinawapa fursa ya kubadilishana mawazo na uzoefu katika masuala yanayohusu elimu .Sera na mipango mbalimbali ikiwemo mpango wa maendeleo ya elimu ya msingi (MMEM) na mpango wa maendeleo ya elimu ya sekondari (MMES) inasisitiza ushiriki wa wananchi katika utekelezaji wake.Hivyo wananchi wote wanawajibu wa kuchangia uboreshaji wa elimu na demokrasia nchini. kujiunga na harakati hizi za marafiki wa elimu ni bure na hakuna malipo yoyote wasiliana nasi kwa namba 0755 65 00 75 au 0786 65 00 75 au e-mail jmrchrd@yahoo.com tukuunganishe na marafiki wa elimu popote ulipo Tanzania

Jumanne, 3 Juni 2014

wanafunzi DIT wagoma kufanya mitihani

Wanafunzi wa Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT) wamegoma kufanya mitihani ya muhula kutokana na wenzao 684 kutopatiwa namba za mitihani kwa madai ya kutokamilisha usajili.

Mgomo huo umesababisha mitihani iliyopangwa kufanyika jana asubuhi na mchana kutofanyika kutokana na wanafunzi hao kugomea kuingia vyumba vya mitihani.

Akizungumza na NIPASHE Rais wa serikali ya wanafunzi, Himida Elihuruma, alisema wamelazimika kugomea mitihani hiyo kwa sababu kuna wanafunzi walifanya usajili tangu Februari, lakini hawajapewa namba za mtihani kwa maelezo kuwa hawajakamilisha taratibu.

“Kuna wanafunzi wamesajiliwa baada ya kukamilisha taratibu zote tangu Februari, lakini  la kusikitisha hawajapatiwa namba kwa kuambiwa kwamba hawajafanya usajili,” alisema Elihuruma.

“Ofisi ya Uhasibu imegubikwa na rushwa, kuna ushahidi wa baadhi ya viongozi na wanafunzi waliombwa ili watafutiwe fomu ambazo zimepotea hali iliyopelekea hadi leo kutopata namba za mtihani,” alisema.

Aidha, alisema kumekuwapo na ubaguzi unaofanywa na utawala kwa kuwanyima namba za mitihani wanafunzi waliokamilisha usajili na kuwapa ambao hawajakamilisha. Aliongeza kuwa uongozi wa chuo umekuwa na utaratibu mbovu wa kupanga tarehe za usajili na kwa mara ya kwanza ilipangwa Machi 7  ikasogezwa Mei 16 hadi 23, mwaka huu bila kutoa taarifa kwa wanafunzi.

Wanafunzi waliohojiwa na gazeti hili walisema hawatafanya mitihani hiyo hadi pale wenzao watakapopewa namba.

Ofisa Uhusiano wa taasisi hiyo, Amani Kakana, alisema mgomo huo hautambuliki na mitihani iliyogomewa jana itapangwa tena na usajili hautaongezewa muda.

“Tulitoa muda wa kutosha wanafunzi kufanya usajili walioshindwa kufanya kwa wakati hawawezi kupatiwa namba, tunafuata utaratibu wa chuo uliopangwa unaoleweka na wanafunzi,” alisema Kakana.

“Mwanafunzi anayejielewa hawezi kugomea mtihani, ratiba haitaharibika itaendelea kama ilivyopangwa, tutamchukulia hatua kali mtu yeyote atakayejaribu kuchochea vitendo vya uvunjifu wa amani,” alisema.

souce ippmedia & nipashe