Kurasa

HARAKATI ZA MARAFIKI WA ELIMU NI NINI?

HARAKATI ZA MARAFIKI WA ELIMU NI NINI?
Ni harakati za watu wanaojali na wenye nia ya kuleta mabadiliko katika kuboresha elimu na demokrasia nchini. Harakati hizi zinawaleta pamoja wananchi wanaopenda maendeleo ya elimu na zinawapa fursa ya kubadilishana mawazo na uzoefu katika masuala yanayohusu elimu .Sera na mipango mbalimbali ikiwemo mpango wa maendeleo ya elimu ya msingi (MMEM) na mpango wa maendeleo ya elimu ya sekondari (MMES) inasisitiza ushiriki wa wananchi katika utekelezaji wake.Hivyo wananchi wote wanawajibu wa kuchangia uboreshaji wa elimu na demokrasia nchini. kujiunga na harakati hizi za marafiki wa elimu ni bure na hakuna malipo yoyote wasiliana nasi kwa namba 0755 65 00 75 au 0786 65 00 75 au e-mail jmrchrd@yahoo.com tukuunganishe na marafiki wa elimu popote ulipo Tanzania

Jumamosi, 21 Septemba 2013

CCM yatoa miezi 6 kwa waziri wa Elimu kujiuzulu....Vinginevyo itamtimua kwa nguvu




CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimemtaka Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa kujiuzulu kwa kushindwa kulipa madeni ya walimu nchini.

Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana pia ametoa muda wa miezi sita kwa Waziri huyo na Naibu wake Philip Mulogo kutekeleza hilo agizo hilo vinginevyo chama kitawatumia wabunge wake kuwatimua kwa nguvu.

Kwa mujibu wa taarifa za madeni zilizokusanywa na Chama cha Walimu Tanzania (CWT), hadi sasa walimu wanadai malimbikizo yao ya Sh bilioni 49 ambayo hajalipwa na Serikali.

Kinana alikuwa akihutubia mikutano ya hadhara jana katika wilaya za Bariadi na Busega.

Alisema CCM haiko tayari kuona walimu wakinyanyaswa wakati wana madai ya msingi.

Hivi sasa imejengeka tabia kwa baadhi ya mawaziri na watendaji wa wizara ya kuwadharau walimu na hata kuwanyanyasa huku wengine wakishusha utu na heshima ya walimu kwa kuwatukana, alisema.

Kinana ambaye yupo katika ziara ya mikoa ya Kanda ya Ziwa alisema kwa mawaziri kushindwa kutatua kero za walimu, imefika wakati wahusika waondoke wenyewe na wasipofanya hivyo chama kitawaagiza wabunge wake wawafukuze kwa nguvu.

“Ninatoa muda wa miezi sita kwa Waziri wa Elimu na wasaidizi wake wakiwamo watendaji kuhakikisha wanalipa madeni ya walimu haraka. Haiwezeni hii ni nchi ya watu wote wakiwamo walimu wadharauliwe na hata kunyanyaswa kwa maneno ya matusi

“Hili hapana CCM haiko tayari kuona walimu kila siku wakipigwa danadana kutokana na uzembe wa watu waliokabidhiwa dhamana za kuongoza sekta ya elimu katika nchi yetu,” alisema.

MTANZANIA ilimtafuta Katibu Mkuu wa CWT, Ezekiah Oluoch ambaye alisema hadi sasa madeni ya walimu yamefikia Sh bilioni 49 ambayo ni malimbikizo ya mishahara na mapunjo.

“Kila mara tunawaambia kuwa ni vema Serikali itafute Sh bilioni 100 katika fungu la dharura ili iweze kulipa madeni ya walimu na iachane nao lakini hawasikii,” alisema Oluoch.

Source: Mtanzania

Chikombe: Shule yenye walimu watatu wanafunzi 300

Nikiwa ziarani mkoani Lindi nafanikiwa kupita katika shule mbalimbali za msingi na sekondari. Lengo hasa lilikuwa ni kuangalia mazingira halisi ya shule hizo kama yanaweza kuleta tija kwa siku za baadaye?

Shule ya msingi Chikombe ndiyo kambi yangu ya kwanza katika ziara hii. Kwa kutumia usafiri wa pikipiki nafanikiwa kufika shuleni hapa saa tano asubuhi, nikitokea Lindi Mjini.

Mbele yangu ni uwanja mkubwa wa nyasi ukiwa na miti michache ya miembe. Kuna wanafunzi wachache wakiwa wamezagaa katika eneo hilo wakicheza mpira. Hii inaashira kuwa wako kwenye muda wa mapumziko.

Kadiri ninavyosogea nazidi kuwa karibu na majengo ya shule mbele yangu. Ni majengo mawili yenye hali tofauti. Moja ni jengo lenye madarasa mawili na ofisi moja ndogo ya walimu linaloonekana kuwa jipya kidogo.

Pia jingine ni jengo kuukuu lililojengwa kwa udongo na miti. Kwa kulitazama jengo hili unaweza kulifananisha na zizi la ng’ombe ama stoo ya kuhifadhia vifaa vya kilimo. Jengo hili lina vyumba vitatu vinavyotumika kama madarasa.

Upana wa chumba kimoja cha jengo hilo unaweza kuwa ni urefu wa madawati mawili na uchochoro wa kupita mtu mmoja katikati.

Wanafunzi wa darasa la awali, la kwanza, la pili la tatu na la nne hutumia madarasa haya kama sehemu yao ya kusomea.

Kwa muda huu nilioingia nakuta wanafunzi wa darasa la kwanza wakiwa katika maandalizi ya kutoka shule.

Nafika kwenye ofisi ya walimu kwa ajili ya kujitambulisha na kupata mwenyeji wangu, ambaye ningepata mawili matatu kuhusiana na shule hiyo iliyo katika Wilaya ya Lindi Vijijini Jimbo la Mtama.

Mwalimu Hassan Halfan (54) ndiye alikuwa wa kwanza kukutana naye. Yeye ni mmoja kati ya walimu watatu katika shule hiyo. Kama ilivyo ada ya mgeni na mwenyeji alianza kwa kunipa historia ya shule yake.

“Shule ya Chikombe ilianza rasmi mwaka 2008 ikiwa na mwalimu mmoja ambaye ni mimi mwenyewe, nikiwa peke yangu niliweza kufundisha kwa miaka miwili bila usaidizi hadi mwishoni mwa mwaka 2009, alipokuja mwalimu mwenzangu,” alisema.

Mwaka 2010 idadi ya walimu iliongezeka na kufikia walimu watatu ambao tupo pamoja hadi hivi sasa.Changamoto kuu zinazoikabili shule hii

Kama ilivyo kwa shule nyingi zilizo katika Mkoa wa Lindi, Shule ya Chikombe inakabiliwa na matatizo lukuki kiasi cha kushindwa kujiendesha ipasavyo.Mradi pekee unaotegemewa katika shule hii ni ule wa shule ya awali, ambapo wazazi hulazimika kuwalipia watoto Sh300 kama ada ya mwanafunzi mmoja kwa mwezi.

“Pamoja na kuwekwa kwa kiasi kidogo cha ada, wazazi wanashindwa kuilipa na hivyo kuzidi kutupa wakati mgumu,” anasema mwalimu Halfani.

Anasema uchache wa walimu nalo ni tatizo linguine, ambapo walimu watatu waliopo wanalazimika kufundisha wastani wa vipindi 64 hadi 75 kwa wiki.
Jambo hili kwa kiasi kikubwa limekuwa likiwapa mtihani walimu hao na hata kushindwa kufanya shughuli zao kwa ufanisi.

“Uchache wa walimu umekuwa ukikwamisha maendeleo ya shule yetu kwa kiasi kikubwa sana. Lakini ukiachikia mbali uchache huo, hapa shuleni kwetu kuna uhaba wa nyumba za walimu,” anasema.

“Katika kipindi cha miezi kadhaa iliyopita, tulilazimika kuwaondoa wanafunzi katika darasa moja ili kumpisha mwalimu mkuu ambaye alikuwa hana nyumba ya kuishi,” anasema mwalimu Halfan.

Jambo hilo lilisababisha msongamano wa wanafunzi katika vyumba vya madarasa, kwani madarasa manne yalilazimika kutumiwa na mikondo saba na wengine ilibidi wafundishiwe nje ya madarasa anasema mwalimu huyo.

Baada ya kuona ukubwa wa tatizo hilo, wanakijiji waliingilia kati na kwa pamoja walishirikiana kujenga nyumba moja ya mwalimu mkuu, ili kuwapa wanafunzi nafasi ya kushiriki masomo darasani.
mwananchi.co.tz