Kurasa

HARAKATI ZA MARAFIKI WA ELIMU NI NINI?

HARAKATI ZA MARAFIKI WA ELIMU NI NINI?
Ni harakati za watu wanaojali na wenye nia ya kuleta mabadiliko katika kuboresha elimu na demokrasia nchini. Harakati hizi zinawaleta pamoja wananchi wanaopenda maendeleo ya elimu na zinawapa fursa ya kubadilishana mawazo na uzoefu katika masuala yanayohusu elimu .Sera na mipango mbalimbali ikiwemo mpango wa maendeleo ya elimu ya msingi (MMEM) na mpango wa maendeleo ya elimu ya sekondari (MMES) inasisitiza ushiriki wa wananchi katika utekelezaji wake.Hivyo wananchi wote wanawajibu wa kuchangia uboreshaji wa elimu na demokrasia nchini. kujiunga na harakati hizi za marafiki wa elimu ni bure na hakuna malipo yoyote wasiliana nasi kwa namba 0755 65 00 75 au 0786 65 00 75 au e-mail jmrchrd@yahoo.com tukuunganishe na marafiki wa elimu popote ulipo Tanzania

Ijumaa, 28 Machi 2014

mwanafunzi bingwa wa hisabati na ndoto za udaktari

Unapomuona kabla ya kuzungumza naye, ni rahisi kuamini kwamba Sunday Mrutu (18) ana hulka ya usikivu, upole na kutafakari kabla ya kutamka ama kuchukua hatua yoyote. Ndivyo ilikuwa wakati nikijiandaa kumhoji, muda mfupi baada ya uongozi wa Shule za St. Anne Marie za jijini Dar es Salaam, kumtunukia Sh milioni tatu, kutokana na mafanikio yake katika mitihani ya kuhitimu kidato cha nne mwaka jana. Mkurugenzi wa Shule za St. Anne Marie, Jasson Rweikiza, Uanamtaja Mrutu kuwa kati ya wanafunzi wawili wa shule hiyo waliopata kati ya pointi saba na tisa za daraja la kwanza, yeye (Mrutu) akiwa na pointi saba. Kwa upande mwingine, Rwekiza akasema Mrutu alikuwa miongoni mwa wanafunzi 10 bora nchi nzima, akishika nafasi ya sita, wakati aliongoza katika utahiniwa uliofanywa na Baraza la Mitihani, kama ilivyo kwa hisabati aliyopata alama 98 kati ya 100. Rwekiza anasema matokeo hayo na mengine hususani yaliyowahusisha wanafunzi 32 wa St. Anne na shule dada ya Brilliant, waliopata daraja la kwanza, yanajenga heshima kwa vijana hao na uongozi wa shule hizo. Tayari uongozi wa St. Anne Marie, Brilliant Sunshine, zote zikimiliwa na Rwekiza, zimetoa jumla ya Shilingi milioni 13.2 kwa wanafunzi waliopata daraja la kwanza. Zawadi hizo ni utekelezaji wa ahadi iliyotolewa na Mkurugenzi wa shule hizo, Rwekiza, kwa wanafunzi waliohitimu kidato cha nne mwaka jana. Wanafunzi hao walipata kiasi tofauti cha fedha ambapo waliofaulu kwa kati ya pointi 15-17 walikuwa 14 na walizawadiwa Shilingi 200,000 kila mmoja. Wengine na kiasi cha fedha alizopata kila mmoja ni 13 waliofaulu kwa kati ya pointi 13-14 (300,000), wanafunzi watano waliofaulu kwa kati ya pointi 10-12 (500,000) na wawili waliopata kati ya pointi 7-9 (1,000,000). Hata hivyo, mwanafunzi aliyekuwa miongoni mwa wawili hao, SundayMrutu alipewa zawadi tofauti kutokana na mafanikio makubwa aliyoyapata katika mitihani hiyo. Mwanafunzi huyo alizawadiwa Shilingi 1,000,000 kwa miongoni mwa wanafunzi 10 bora nchini ambapo alishika nafasi ya sita huku akiwa wa kwanza kwa upande wa wavulana. Pia Mrutu alizawadiwa Shilingi 500,000 kwa kuwa wa kwanza kwenye utahiniwa uliofanywa na Baraza la Mitihani la Taifa na kiasi kama hicho kwa kuongoza katika somo la hisabati nchi nzima, ambapo alipata alama 98. Rwekiza, akasema ingawa fedha hizo zinaweza kuonekana kuwa nyingi, lakini zitasaidia kuibua na kuhamasisha ari ya usomaji kwa wanafunzi wa shule hizo na nyingine nchini. “Tunalolifanya hapa kwa kutoa zawadi hizi za hamasa ni jambo la kawaida kwa kila mwaka, lengo kubwa hapa ni kuhakikisha watoto wetu wanaamini kwamba ahadi tunayowapa kuhusu kusoma kwa bidii zinatekelezwa,” anasema. Mrutu anathibitisha kwamba hisabati ni moja ya masomo anayoyamudu darasani, hali hiyo ikichochewa na umakini, usikivu na uelewa pindi mwalimu anapofundisha darasani. “Hisabati inaaminika kuwa somo gumu sana, lakini ninaamini kwamba kama mwanafunzi atakuwa msikivu, atatulia na kufuata mafundisho ya mwalimu, itakuwa kinyume chake….hisabati ni somo zuri na linaloeleweka kwa urahisi,” anasema. Mrutu anakumbuka namna alivyowafuatilia na kuwatii walimu wake waliowahi kumfundisha hisabati, akiwataja kwa jina moja moja kuwa Tarimo, Tino na Samuel. Wakati Mrutu akisema hivyo, wanafunzi wa shule kadhaa za sekondari wamekuwa wakilielezea somo hilo kama moja ya masomo yanayowashinda katika kusoma na kufaulu. KUHUSU UFAULU WAKE Mrutu anasema hadi matokeo ya kidato cha nne yalipotoka na kutaarifiwa kuhusu ufaulu wake, hakuamini kwa urahisi. “Nilifuatwa nyumbani (bila kumtaja mtu aliyemfuata) na kuambiwa kwamba nimefanikiwa vizuri sana kwenye mitihani yangu,” anasema. ANAPENDELEA UDAKTARI Mrutu anasema pamoja na kuwa na uwezo unaomfanya alimudu vyema somo la hisabati, kusudio lake ni kutaka kusomea Udaktari. “Ninajua hisabati ni somo muhimu lisilopewa kipaumbele sana kwa madaktari, ila mimi nafsi yangu ni kuona ninasoma kufikia kuwa Daktari wa binadamu,” anasema. CHANGAMOTO KWA WANAFUNZI SHULENI Mrutu, anasema ni jambo lililo wazi kwamba katika maisha ya takribani miaka minne ya kusoma sekondari ya awali, wanafunzi wanajenga urafiki na uhusiano wa karibu. Hata hivyo, anasema kinachotakiwa kwa mwanafunzi ni kuweka mipaka ya urafiki na uhusiano, kisha kusimamia dhamira, nia na utashi vinavyomuongoza. Anasema kukosekana kwa mipaka katika urafiki na uhusiano, ni miongoni mwa vyanzo vya kuibuka tabia zisizofaa, nyingi kati ya hizo zikitokana na kujifunza kunasababishwa na muingiliano wa kirafiki ama kimahusiano. “Sasa inapokuwa kwamba mpo marafiki wengi shuleni na huwezi kuwakimbia, ni vizuri mwanafunzi ukajiepusha na kuiga mambo, vinginevyo utajikuta unaachwa na wale uliokuwa unawaiga, kwa maana kila mtu ana mbinu zake,” anasema. CHANZO: NIPASHE JUMAPILI

Jumatano, 19 Machi 2014

madarasa walimu na vitabu bado changamoto

Shule ya sekondari Tongoni mkoani Tanga ina majengo mazuri, walimu 12, maabara, vitabu lakini kitaifa inashika nafasi ya tatu kutoka mwisho katika matokeo ya kidato cha nne mwaka jana. Shule hiyo, ina walimu 12 wengi wao wakiwa na elimu ya kiwango cha shahada ya elimu. Ina madarasa manane, madawati kwa kila mwanafunzi, maabara na vitabu vya kutosha. Tangu kuanzishwa kwake mwaka 2007 haijafaulisha mwanafunzi hata mmoja kwa kiwango cha daraja la kwanza, la pili wala la tatu. Daraja la kujivunia kwa shule hiyo kwenye mitihani ya kidato cha nne ni la nne na sifuri kwa watahiniwa wake. Sasa shule hiyo ina wanafunzi wapatao 123 kati yao wasichana ni 52 na wavulana 71. “Ni wanafunzi watatu tu kati ya 47 walioweza kufaulu mtihani wa kidato cha pili mwaka juzi … shule ikalazimika kuwatafutia wanafunzi hao shule nyingine ili waendelee na masomo. Waliobaki wakalazimika kurudia kidato cha pili,” alisema Mwalimu Mkuu wa shule hiyo, Mfaume Juma. Mwalimu Juma anasema mwaka jana, watahiniwa wa kidato cha nne walikuwa 37 wanafunzi saba kati yao hawakupata matokeo yao kwa kushindwa kukamilisha ada ya mtihani na 28 wakaambulia daraja sifuri. Ni wawili tu walipata daraja la nne. “Mwaka jana wanafunzi 28 walipata daraja sifuri katika mtihani wa kidato cha nne, saba matokeo yao yalizuiwa na Baraza la Mitihani la Taifa kwa kushindwa kulipa ada ya mtihani,” anasema Mwalimu Mkuu huyo. Miongoni mwa changamoto zinazoikabili shule hiyo, Mwalimu Mkuu anazitaja kuwa ni mwamko mdogo wa baadhi ya wazazi kuhusu umuhimu wa elimu hasa ulipaji wa ada na michango ya shule bado ni tatizo kubwa. Hatua hiyo, anasema inasababisha shule hiyo kushindwa kujiendesha kikamilifu asilimia 75 ya wanafunzi wanadaiwa ada. Changamoto nyingine ni ukosefu wa nyumba za walimu na mabweni kwa wanafunzi. Asilimia 70 ya wanafunzi wa shule hiyo huishi nje ya eneo hilo. “Kutokana na ukosefu wa nyumba za walimu na mabweni kwa wanafunzi baadhi ya wanafunzi wanachelewa kufika shule… kuna wanafunzi wanaoishi katika kisiwa cha Mwarongo ambacho ili kufika ng’ambo ya pili lazima wavuke kwa mashua.Wakati mwingine hutegemea hali ya upepo wa bahari siku ukivuma vibaya watoto wanashindwa kufika shuleni,” anafafanua Mwalimu Juma. Baadhi ya wanafunzi wa shule hiyo wanasema, wamekuwa wakishindwa kuhudhuria masomo kwa wakati au kuchelewa hasa siku ambazo hali ya upepo wa bahari ukiwa mbaya. “Mimi huwa naamka nyumbani saa 11 alfajiri, kuosha vyombo na kuchota maji baada ya hapo najiandaa kwenda shule, lakini ukifika Kivukoni ni lazima usubiri maji yajae ndiyo chombo kiweze kuvuka. Siku ambazo upepo ni mbaya mara kadhaa tulishawahi kuzama, hali iliyotulazimu baada ya kunusurika turudi nyumbani badala ya kwenda shule. Hii inatuumiza na kutuathiri sana kimasomo,” anasema Mariam Hassan mwanafunzi wa kidato cha kwanza shuleni hapo. Naye Zuberi Hamid, mwanafunzi wa kidato cha tatu shuleni hapo anasema, imekuwa ni kama kawaida kwao kutohudhuria vipindi viwili vya kwa asubuhi kutokana na hali ya usafiri kuwa ya mashaka na kimsingi hali hiyo imekuwa ni njia mojawapo inayochangia kufeli masomo yao. “Muda tunaoingia shuleni ni saa nne asubuhi unakuta vipindi viwili vya mwanzo vimekamilika. Pia muda tunaotoka shule nao hadi kuvuka na kufika nyumbani tunachelewa.Tukifika nyumbani muda unakuwa umekwenda sana hata fursa ya kujisomea inakuwa finyu sana, “ anasema Hamid. Baadhi ya walimu wanasema , shule hiyo yenye walimu 12 kati yao hakuna waliobobea katika masomo ya Biolojia, Fizikia na Hisabati hali inayowalazimu wanafunzi kufanya mitihani ya masomo hayo bila kufundishwa. “Kwa sababu ya kutokuwa na walimu wa Physics,Hesabu na Biology wanafunzi wanalazimika kufanya mitihani bila kufundishwa masomo hayo hili nalo ni tatizo sana,” anasema Thomas Simengwa, Mwalimu wa somo la Historia na Kiswahili katika shule hiyo. Omary Bushiri ni Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji cha Tongoni anakiri kuwepo mwamko mdogo wa wazazi katika uchangiaji wa sekta ya elimu kijijini hapo sambamba na mmomonyoko wa maadili kwa baadhi ya wanafunzi wa shuleni hiyo. Bushiri ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya shule hiyo, anasema changamoto kubwa inayoikabili shule hiyo pamoja na mambo mengine ni mawasiliano duni kati ya uongozi wa shule, wazazi na wanafunzi. “Ni ukweli kabisa kwamba maendeleo ya shule ya sekondari Tongoni yamekuwa yakididimia siku hadi siku lakini tatizo lipo kwa pande zote tatu kwa maana ya uongozi wa shule, wanafunzi, walimu na bodi ilishaomba uongozi wa shule kuandalia mkutano na wanafunzi lakini hadi leo jambo hilo halijafanyika ,“ anasema Bushiri. Anasema lengo la Bodi ya shule kutaka kukutana na wanafunzi wa shule hiyo ni baada ya kufahamishwa kuwa walimu wamekuwa na tabia ya kutoingia darasani kwa wakati na wengine kuishia njiani bila kufika shule na tabia nyingine ambazo ni kinyume cha maadili ya wanafunzi. “Wanafunzi walishalalamika kwamba walimu hawaingii darasani kwa wakati….lakini si hilo tu, pia wanafunzi wenyewe wana matatizo yao mengi tu ujana umewazidi na ndio maana tulitaka kuzungumza nao,” anasema. Anasema anashangaa wanafunzi kuchelewa shule kwa kisingizio cha usafiri wa mashua wakati kuna boti inayowasafirisha bila kikwazo chochote na kwamba hilo ni tatizo na uzembe wa ufuatiliaji wa wanafunzi kati ya uongozi wa shule na wazazi. Ofisa Mtendaji wa Kata ya Tongoni, Luis Makame anasema wakazi wa kata hiyo hawana mwamko katika uchangiaji wa masuala ya elimu wakiamini kuwa elimu ya msingi inatosheleza kuendesha maisha ya watoto wao. “Kusema kweli, changamoto kubwa hapa ni uelewa wa wazazi katika kuchangia sekta ya elimu.Wengi wanaamini kuwa, kila mtoto ana riziki yake na kwamba elimu ya msingi inatosha kabisa kuendesha maisha ya watoto wao ya kila siku, “ anasema Makame. Kwa upande wao, baadhi ya wazazi wa Kata ya Tongoni wakizungumzia hali hiyo wanatupia lawama uongozi wa shule na kusema kuwa umeshindwa kuwafuatilia wanafunzi wao na baadhi wamekuwa na mienendo isiyofaa. Selemani Sharif ni mmoja wa wazazi, ambaye anasema kuwa, licha ya walimu kutoa malalamiko ya wazazi kutochangia ada kikamilifu, lakini nao wameshindwa kusimamia uendeshaji wa shule kwani hata wanafunzi nao wanalalamikia walimu kutoingia madarasani kwa wakati. “Sisi wazazi tunalaumiwa hatutaki kuchangia maendeleo ya shule, lakini walimu nao wanalalamikiwa na wanafunzi kutoingia madarasani na si hilo tu, uongozi wa shule umeshindwa kusimamia tabia za wanafunzi wao ambao tunawakuta vichochoroni wakati wa masomo na hiki kichaka ndiyo gesti yao, walimu wanakuwa wapi wakati huo hata wanafunzi wazurure ovyo,” anahoji Sharif. Naye Mwajuma Mwanajumaa anaiomba serikali kufanya mabadiliko ya uongozi wa shule hiyo kwa sababu wazazi hawaridhishwi na matokeo ya shule hiyo. “Shule hii wakati ikijengwa wananchi tuliichangia…kuitokana na umuhimu wake kama kweli hatupendi elimu ilikuwaje tulitoa nguvu zetu hadi ikajengwa…walimu na uongozi wa shule umetukatisha tamaa sana… sasa ili twende vizuri tunaiomba serikali iingilie kati suala hili,” anasisitiza Mwanajumaa. Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Tanga ambaye pia ni Ofisa elimu Sekondari wa Jiji hilo , Bashiri Shelimo anasema hatua ya kwanza itakayochukuliwa ni kuuondoa uongozi mzima wa shule hiyo. Shelimo anasema, hatua ya pili ni kuhamisha walimu wa shule hiyo na kuwapeleka walimu wapya sambamba na kuunda upya bodi ya shule hiyo. Anasema changamoto kubwa inayoikabili shule hiyo hadi kufikia katika hali hiyo mbaya ni uongozi mbovu uliodumu kwa muda mrefu unaofanya kazi kwa mazoea. “Nina miezi kadhaa tangu nilipohamia hapa lakini kwa uchunguzi wangu wa awali nimeona kuna haja ya kuupangua uongozi wa shule hiyo. Bahati nzuri Mwalimu mkuu mwenyewe aliomba yeye na makamu wake wapumzishwe na tukaona ni sababu za msingi ili kuleta mabadiliko chanya kwenye shule ile,” anafafanua Ofisa elimu huyo. CHANZO: NIPASHE

Jumapili, 16 Machi 2014

Baadhi ya wanafunzi wa kiume katika shule za msingi wilayani Kibaha, Pwani, wamejiingiza katika vitendo vya kujaamiana wenyewe kwa wenyewe na watu wengine kutoka nje ya shule na kufikia hatua ya kupasua kaptula zao makusudi ili kurahisisha vitendo hivyo. Shule hizo zipo katika mji wa Mlandizi mkoani humo na vimesababisha wanafunzi hao kuporomoka kimasomo kwa kuwa wanatumia muda mwingi kukaa machimbo ya mchanga na vichakani kwa ajili ya kufanya vitendo hivyo. Katika uchunguzi uliofanywa na NIPASHE imebainika vitendo hivyo hufanywa nyakati za asubuhi wakati vipindi vya masomo vinaendelea na jioni mara wanapotoka shuleni. Kutokana na kukithiri kwa vitendo hivyo, mahudhurio ya wanafunzi kwenye shule hizo yamekuwa ya kusuasua na kusababisha walimu kuwa na kazi ya ziada ya kutafuta ufumbuzi wa tatizo hilo. Uchunguzi huo umefanywa katika shule za msingi za Mtongani, Azimio na Jamhuri zote zipo ndani ya mji huo wa Mlandizi. HALI HALISI Katika hali inayoonyesha kuwa ni mbaya kwenye shule hizo, baadhi ya wanafunzi wameonekana kuathirika kisaokolojia na kupungukiwa na uwezo wa kimasomo darasani. Hata hivyo, afya za wanafunzi hao zipo hatarini kutokana na hofu ya kuambukizwa magonjwa ya zinaa ukiwamo Ukimwi baada ya watu wazima kuhusishwa kuwaingilia. Baadhi ya walimu wa shule hizo walipozungumza na gazeti hili walikiri kuwapo kwa vitendo hivyo na kwamba vimeongezeka kwa kasi ya kutisha na kuwapa hofu. Walisema walengwa wa vitendo hivyo ni wanafunzi kuanzia darasa la tatu hadi la nne ambao mara nyingi wanalazimishwa kulawitiwa na wanafunzi wenzao wa madarasa ya juu. Aidha imedaiwa wanafunzi wengine wanafanyiwa vitendo hivyo na watu wazima wakiwa nyumbani kwao na kwenye mabanda ya kuonyesha picha za video nyakati za usiku. "Tatizo hili limekuwa kubwa, walimu tumejitahidi kupambana nalo kwa kiasi kikubwa lakini inaonyesha hatujafanikiwa," alisema Mwalimu Jamila Kipengele wa Shule ya Msingi Mtongani. Mwalimu Kipengele ambaye anaongoza kitengo cha taaluma, alisema vitendo hivyo vinafanyika katika maeneo hayo ambapo huko wanafunzi wanakutana mara wanapofanikiwa kutoroka wakati wa vipindi vya masomo. "Tunavyosikia huko machimbo wanakuwa watoto kutoka shule tofauti na kutendeana matendo hayo machafu, baada ya kugundua jambo hilo tuliamua kufanya msako mkali wa kuwakamata wote wanaohusika na kuwarudisha shuleni," alisema Kipengule. Kwa shule ya Azimio, Mwalimu Emmanuel Mwambeja ambaye anafundisha darasa la tatu, alieleza nusu ya wanafunzi 98 wa darasa lake hawaingii darasani katika vipindi vya jioni na badala yake wanaishia kwenye machimbo. Mwalimu Tetula Kessy wa Shule ya Msingi Azimio, ambaye yupo kwenye kamati ya kuzuia unyanyasaji wa watoto chini ya Plan Tanzania, alisema wanafunzi wengi wanajikuta wakiingia katika vitendo hivyo kutokana na kushawishiwa na watu wazima na kuangalia picha za ngono kwenye mabanda yaliyozunguka kila eneo kwenye shule hizo. "Tunapokaa na kuwauliza kwa nini wanafanya hivyo, wanajibu kwamba walikuwa wakifanyiwa nyumbani au wanaona kwenye vibanda vya video na wao wanajaribu kwa wenzao," alisema Mwalimu Kessy. WATOTO WAPASUA KAPTULA ZAO Katika Shule ya Msingi Jamhuri baadhi wanafunzi wameeleza upo wakati wanafunzi walifikia hatua ya kupasua kaptula zao upande wa nyuma ili kurahisisha kuingiliwa na wenzao. Baadhi ya wanafunzi ambao majina yao yanahifadhiwa, walisema wanafunzi hao walikuwa na kawaida kwenda kwenye korongo lililo jirani na shule hiyo na kisha kulawitiana. "Wanachana kaptula sehemu ya nyuma kwa kutumia wembe, tulikuja kugundua wanaporudi darasani wanakuwa katika hali tofauti ndipo tukaamua kuripoti kwa walimu," alisema mwanafunzi mmoja. Kauli za wanafunzi hao ziliungwa mkono na Mratibu wa Elimu Kata ya Kilangalanga, Thomas Tito, ambaye alisema amefanya juhudi kubwa kupambana nalo wakati alipokuwa Mwalimu Mkuu katika shule hiyo. "Nakumbuka nilipokuwa naongoza shule hiyo niliwakuta wanafunzi wamepasua kaptula zao kwa nyuma na wembe, nilipodadisi niligundua wanafanya mchezo huo hatari kwa sababu wanapotoka huko vichakani wanakuwa wamechafuka sana," alisema. Kufuatia hali hiyo aliamua kuripoti katika vyombo vya sheria kwa ajili ya kuchukuliwa hatua lakini ilishindikana baada ya kuonekana watoto hao walikuwa wakilawitiana wenyewe kwa wenyewe. "Polisi walishindwa kuendelea kufuatilia na kuachia jukumu hilo uongozi wa shule, nilichofanya niliwaita wazazi kuwaeleza jambo hilo pamoja na kuwachukulia hatua ya kinidhmu wahusika," alisema mwalimu Tito. MABANDA YA VIDEO Hata hivyo, taarifa za uhakika zinaeleza kwamba kinachoendelea ndani ya mabanda ya video yaliyotapakaa kila kona ya mji wa Mlandizi, ni mambo ya kutisha. Imeelezwa kwamba ndani ya mabanda hayo, wamiliki wanaweka picha za ngono bila kujali muda wala umri wa wateja wao, kinachotokea wanaume watu wazima wanawachukua watoto waliokuwamo ndani na kuwaingilia kinyume na maumbile. Baadhi ya wanafunzi waliotoa ushuhuda huo (majina yamehifadhiwa) walisema mara picha hizo zinapoonyeshwa, wanaume hao wanawadanganya watoto kwa kuwapa pesa kidogo na kisha wanawapakata na kuwaingilia. "Kule watu wakubwa wanapakata watoto halafu wanawavua nguo kuwafanyia mambo mabaya," alisema mwanafuzi mmoja. Wanafunzi wengine mara baada ya kuangalia picha hizo, wakienda shuleni wanawachukua wanafunzi wenzao na kwenda kuwafanyia jambo hilo. "Tuna mwanafunzi mwezetu hapa shuleni (jina analitaja) amekuwa na tabia ya kuwaingilia wenzake kinyume na maumbile," alisema mmoja wa wanafunzi hao. Akizungumzia suala hilo, Mwalimu Kipengele alisema kinachozungumzwa na wanafunzi hao ni jambo la kweli, tayari wamembaini mtoto huyo na kumchukulia hatua ikiwamo kuwaita wazazi wake. "Mwanafunzi huyu mahudhurio yake ni mabaya sana, tulipomfuatilia na kumbana sana alikiri kuhusika, na watoto waliofanyiwa vitendo hivyo walijitokeza tunaendelea kuwapatia ushauri nasaha,"alisema Mwalimu Kipengele. Aliomba serikali kuangalia upya utoaji vibali vya kuendesha biashara hiyo, kwani kuna hatari wanafunzi wengi wakaathirika na vitendo hivyo na kuambukizwa Ukimwi pamoja na kushuka kiwango cha elimu kwa ujumla. Hata hivyo wamiliki wa mabanda hayo wanapinga kauli hizo kwa kusema vibali vyao vimewapa masharti ya kutoonyesha picha za aina hiyo, endapo kuna watu wanafanya hivyo basi hawaendeshi biashara zao kihalali. Twaha Linde ambaye alikutwa akionyesha video katika banda lililojengwa jirani na shule ya Msingi Mtongani, alisema kwa upande wake hajawahi kuonyesha picha hizo. Pamoja na utetezi huo, ndani ya banda hilo walikuwapo wanafunzi zaidi ya 10 wa shule tofauti wakifuatilia picha, licha ya muda huo wa saa 6:00 mchana walitakiwa kuwapo darasani. WAZAZI LAWAMANI Walimu wamelaumu wazazi kwa kutokuwa na utaratibu mzuri wa kufuatilia maendeleo ya watoto wao kila siku. Walisema hata wanapopewa taarifa ya watoto wao kutofika shule au kuhusishwa na tabia hizo wanawakingia kifua na kuwa wakali. "Inakuwa tabu pale tunapowapa taarifa wazazi juu ya tabia za watoto wao, mara nyingi wanakuja wakiwa wakali na kusema tunawaongopea, mara nyingi inabidi kutumia mbinu za kuwahoji mbele yao na wanapobaini kuna ukweli wanabaki wakilia," alisema Mwalimu Tito. Aliomba wazazi kuwa na taratibu ya kuchunguza tabia za watoto wao na kufuatilia maendeleo yao ya kielimu kwa ajili ya kuwajengea maadili mema. "Sisi tunasaidia kurekebisha pale wanapokuja shuleni, lakini wakiwa nyumbani hawana udhibiti na ndiyo maana hali hii inazidi kuongezeka huku wazazi hawana habari," aliongeza kusema. Hata hivyo Zuhura Yusufu (30) mkazi wa Mlandizi, alisema kinachosemwa na walimu wa shule hizo kina ukweli kwani wazazi wengi hawawajibiki ipasavyo katika malezi ya watoto wao. Alisema kuibuka kwa hali hiyo kutawazindua wazazi wenzake kwa kuanza kuwafuatilia watoto mara kwa mara OFISA ELIMU ANENA Ofisa Elimu wa shule za Msingi wa Wilaya ya Kibaha, Winfrida Mbuya, alipozungumza na NIPASHE Jumapili, alisema suala hilo limeenea katika shule nyingi na kuwa la kijamii kutokana na wanaohusika hutoka ndani ya familia. Alisema ofisi yake inaandaa tathmini ya jumla kujua ukubwa wake ili kuandaa mkakati wa ufuatiliaji kwa kuchukua hatua mbalimbali ikiwamo kutoa elimu ya ushauri kwa watoto walioathirika. "Ni vizuri tukashirikiana pamoja kuwatambua watoto walioathirika ili waweze kupewa ushauri na wale waliohusika na unyama huo kuchukuliwa hatua za kisheria," alisema. RC: IMENISHTUA SANA Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mwamtumu Mahiza, amesema ameshtushwa na jambo hilo, na kwamba atakahakikisha anakutana haraka na viongozi wenzake kulifuatilia. Alisema yeye kama kiongozi wa juu katika eneo hilo hataweza kuzungumza chochote kabla ya kukutana na wenzake. "Mimi nimeshtuka sana lakini sitaweza kusema kitu kwa sababu bado viongozi wenzangu ngazi ya Wilaya na Halmashauri sijakutana nao, nipe muda nitatoa tamko langu," aliongeza kusema.

Alhamisi, 13 Machi 2014

siri ya kufanya vibaya matokeo ya kidato cha 4 kwa shule za serikali

Miongoni mwa habari zilizoripotiwa katika gazeti hili jana ni pamoja na ripoti maalum iliyofichua baadhi ya sababu za kufanya vibaya kwa wanafunzi wa moja kati ya shule 10 za sekondari zilizoburuta mkia katika mtihani wa taifa wa kidato cha nne uliofanyika mwaka mwishoni mwa 2013. Katika shule hiyo iitwayo Mvuti, iliyopo kwenye Kata ya Msongola, Manispaa ya Ilala jijini Dar es Salaam, ni mtahiniwa mmoja tu aliambulia daraja la tatu. Wengine watatu walipata daraja la nne huku 40 waliobaki wakipata daraja sifuri na mwishowe shule hiyo ikashika nafasi ya 3,251 kati ya 3,256 zilizokuwa kwenye kundi la sekondari zenye watahiniwa 40 au zaidi. Ripoti hiyo inaonyesha kuwa shule ya Mvuti ina changamoto nyingi zinazokwaza maendeleo yao kitaaluma. Uwezo mdogo wa wanafunzi wanaoripoti katika shule hiyo, ukosefu wa vitabu vya ziada na kiada, tatizo la usafiri, njaa kwa wanafunzi na pia kukosekana kwa mkuu wa shule ni baadhi ya matatizo yanayoikwamisha shule hiyo. Sisi tunaona kuwa matatizo haya lukuki yanayoikabili Mvuti yanapaswa kutafutiwa ufumbuzi haraka. Ni wazi kuwa hatua sahihi zisipochukuliwa sasa, Mvuti na shule nyingine za umma zenye changamoto zinazofanana nayo zitaendelea kupata matokeo mabaya katika kila mwaka; jambo ambalo halipaswi kuachwa hivi hivi. NIPASHE tunajua kuwa nyingi kati ya changamoto zinazoikabili Mvuti na shule nyingine za aina yake zinaweza pia kushughulikiwa na uongozi wa shule husika. Halmashauri za manispaa na wilaya ambazo ni miongoni mwa wamiliki wa shule hizi, zinapaswa pia kutekeleza majukumu yao kwa ukamilifu, sawa na serikali kuu na wadau wengine wa sekta ya elimu nchini. Jambo muhimu ni kuwa na dhamira ya dhati kwa kila upande, kwa maana ya viongozi wa shule, wanafunzi, wazazi, serikali na wadau wengine. Kwa mfano, inaelezwa kuwa awali, Mvuti haikuwa na bodi kwa miaka miwili. Hili ni tatizo linalochangia kuwapo kwa matokeo mabaya kwani kupitia bodi, ndipo shule huwa na fursa nzuri ya kujiwekea malengo na kuyasimamia. Lipo pia tatizo la usafiri na njaa. Baadhi ya wanafunzi wa Mvuti hulazimika kupanda mabasi sita hadi nane kwa safari ya kutoka nyumbani kwenda shule na kurudi, achilia mbali safari nyingine ya kutembea kwa miguu umbali wa takriban kilomita nane kwa safari mbili kutoka katika kituo cha mabasi cha Mvuti hadi shuleni kwao. Matatizo ya aina hii huwakabili pia wanafunzi wa shule nyingine nyingi zilizo pembezoni mwa miji. Shule hiyo pia hukabiliwa na tatizo la kupokea baadhi ya wanafunzi wasio na uwezo darasani. Ripoti inaonyesha kuwa asilimia 70 ya wanafunzi walioripoti mwaka 2011 ili kuanza kidato cha kwanza walikuwa hawajui kusoma wala kuandika. Aidha, inaelezwa kuwa ni wanafunzi watatu tu ndiyo waliofaulu kwenye mtihani wao wa kidato cha pili miongoni mwa wale waliofeli sana mwaka huu na kuifanya shule ya Mvuti iingie katika orodha ya shule 10 zilizofanya vibaya. Ni wazi kuwa kama taratibu zingefuatwa, shule hiyo isingepata matokeo hayo mabaya kwani wale waliofeli kidato cha pili wangepata nafasi ya kukariri darasa na wala siyo kuvushwa kirahisi na mwishowe kushusha ufaulu wa shule hiyo. NIPASHE tunaamini kuwa bodi ya shule ya Mvuti, kwa kushirikiana na wazazi wa wanafunzi na wadau wengine wa elimu, wanaweza kubuni utaratibu mzuri wa kukabiliana na tatizo la usafiri, maji na chakula kwa watoto wao. Mipango ya kujenga mabweni zaidi kwenye shule za pembezoni kama Mvuti ni muhimu. Aidha, Wizara ya Elimu inapaswa kuangalia vyema mfumo wake wa kuwapima watahiniwa wa darasa la saba ili wanafunzi wote wanaochaguliwa kujiunga kidato cha kwanza wawe na sifa sahihi kwani ni vigumu sekondari hizi za kata kupata matokeo mazuri ikiwa zitaendelea kupokea wanafunzi wasiojua kusoma wala kuandika. Njia pekee ya kuzikomboa shule za kata kama Mvuti ni kushughulikia kero zilizopo. Kwa kufanya hivyo, nazo zitaimarika na kupandisha viwango vyao vya ufaulu.

Ijumaa, 7 Machi 2014

kauli ya Kawambwa yawachefua walimu

waziri wa elimu dk. shukuru kawambwa
Chama cha Walimu Tanzania (CWT) kimekerwa na kauli ya Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa , kuwa serikali inaendelea kujadiliana na taasisi za fedha juu ya namna ya kulipa deni la malimbikizo ya mishahara ya  walimu yanayofikia Sh. bilioni 61.

CWT  imesema kauli hiyo ya serikali ni kutafuta visingizio baada ya  kushindwa kutekeleza ahadi yake kuwa ifikapo Februari, mwaka huu deni la walimu litakuwa limelipwa.

Rais wa CWT, Gration Mkoba,  alisema hayo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana.

Alisema majadiliano ya mishahara ya walimu yalitokana na mgomo wa  2012 baada ya kukaa kwenye meza ya majadiliano na serikali ilikubali kulipa deni na kuandaa utaratibu wa kupandisha walimu madaraja.

“Inasikitisha kuona majadiliano yanahusisha waandishi wa habari bila ya kujua kuwa kwa kauli yake waziri tayari  walimu wameingia kwenye mgogoro na serikali, lakini  nawasihi walimu wasubiri tamko rasmi la mgogoro,” alisema.

Mkoba alisema tangu serikali ilipoahidi kutekeleza madai yao, hakuna hata dai moja  lililotekelezwa  lakini imewashangaza kuona ikijinadi kuwa inaendelea na majadiliano ya kulipa deni hilo wakati majadiliano hayana tija kwa mwalimu.

Alisema Novemba, mwaka jana mkutano mkuu wa CWT ulitoa siku 60 kwa serikali kukamilisha taratibu zote la kulipa malimbikizo ya mishahara ya walimu nchini.

Pia Januari mwaka huu kwenye kikao cha Baraza  la Taifa la CWT kiliazimia kuwa ifikapo mwishoni mwa Februari, mwaka huu, ikiwa serikali itashindwa kulipa malimbikizo hayo litakuwa tayari kuongoza mgomo.
CHANZO: NIPASHE

bunge la katiba lakiuka katiba ya tanzania ibara ya 18

Bunge  la Katiba limeamua kuweka kitanzi kwa uhuru wa wananchi kupata habari za mchakato wa Katiba Mpya, kwa kuwazuia waandishi wa habari kuingia kwenye Kamati 12 za wajumbe wa Bunge hilo zitakazojadili Rasimu ya Katiba.

Mjadala mkali ulizuka kwa juzi na jana kwenye Bunge hilo, huku baadhi ya wajumbe wakitaka uhuru wa wananchi kupata habari uwapo kwa waandishi kuruhusiwa kuingia kwenye kamati na wengine wakiwamo wajumbe wa Kamati ya Kanuni na Kumshauri Mwenyekiti wakipinga vikali kwa kutaka waandishi wapewe taarifa kutoka kwa mwenyekiti wa kamati husika.

Kifungu cha 57 fasili ya kwanza ya Kanuni za Bunge Maalum la Katiba, kinaeleza kuwa vikao vyote vya kamati vitakuwa vya faragha na hakuna mtu yeyote asiyekuwa mjumbe wa kamati, mtumishi wa Bunge au mtaalam aliyeitwa na Mwenyekiti wa Bunge Maalum atakayeruhusiwa kukaa katika sehemu yoyote ya ukumbi wa mikutano ya kamati wakati kikao cha faragha kinaendelea.

Fasili ya tatu, inaeleza kuwa bila kuathiri masharti ya kanuni hii Mwenyekiti wa Kamati ya mjumbe yeyote kwa idhini ya Mwenyekiti anaweza kutoa taarifa kwa vyombo vya habari kuhusu mambo yaliyojitokeza kwenye kikao cha kamati.

Baadhi ya wajumbe waliiomba kuwasilisha mapendekezo yao kwenye kifungu hicho, walitaka waandishi wa habari kuruhusiwa kwani kwa kuwazuia ni kwenda kinyume cha ibara ya 18 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano inayotaka kuwapo kwa uhuru wa kupata taarifa.

OLUOCH
Ezekiel Oluoch alisema anashauri vikao viwe wazi kwani hakuna jambo la siri la kujifungia kwani wananchi wana haki ya kujua kinachojadiliwa kwenye kamati na kwamba ni vyema kamati zikawa huru.

HALIMA MDEE
Halima Mdee alisema wenye jukumu la kuzitengeneza kanuni ni wajumbe na kwamba awali kamati ya kanuni na kumshauri mwenyekiti baada ya majadala mkubwa kamati ilipendekeza waandishi waruhusiwe kuingia kwenye vikao, na ikakubaliwa kwenye vikao vya kamati ambavyo vitakuwa na mijadala mikubwa na watakapokuja kwenye Bunge watafanya majumuisho kwenye manbo yaliyojadiliwa.

“Tulikubalina watu watakaokatazwa ni wananchi wa kawaida kutokana na
udogo wa kumbi, ila waandishi wa habari wakubaliwe, sisi ndiyo tunaopitisha kanuni na sisi tuliridhia ilikuwa ni matarajio yetu,”
alisema.

Alisema waliotajwa kwenye kanuni waruhusiwe kuingia na utaratibu utakaotumika uamuliwe na mwenyektii wa kamati kushauriana na makamu mwenyekiti.

“Waandishi wa habari waingie mnaogopa nini, mnaficha nini?...hii Katiba ni ya wananchi wana haki ya kujua kila kinachoendelea ndani ya kamati na nje ya kamati na kwenye ukumbi wa Bunge,” alisema Mdee.

MOSES MACHALI

Moses Machali alipendekeza fasili ya tatu ya kifungu hicho, ifutwe kwa kuwa inaweka kitanzi kwa uhuru wa wananchi kupata habari na hakimlazimishi mwenyekiti au makamu kutoa taarifa kwa waandishi wa habari.

Alisema vikao vyote vifanyike kwa uwazi bila kuzuia mtu ingawa hawataruhusiwa kushiriki kwenye mjadala wa kamati.

“Hao wanaosisitiza kura ya wazi halafu mnaogopa na kuwakataa waandishi wa habari mnaficha nini, sioni sababu ya msingi,” alisema Machali.

MARIA SARUNGI
Maria Sarungi alisema vikao vya kamati viwe wazi kwa waandishi wa habari kwa kuwa Rasimu ya Katiba itakwenda kwao kwa ajili ya kuipigia kura.

“Mwanzo wa Rasimu ya Katiba unasema kwakuwa sisi wananchi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tumeamua...Katiba hii si ya kwetu tuliokaa humu ndani bali ya wananchi wa Tanzania, mchakato ulivyoanza ilianza kwa wananchi hadi tulipofika,” alisema.

FREEMAN MBOWE
Freeman Mbowe alisema Katiba inayotungwa ni ya wananchi na wanaowakilishwa ndani ya Bunge hilo wanataka kujua kila kinachoendelea ndani ya Bunge hilo.

“Tusifikiri tunahitaji kuridhiana sisi wenyewe tulioko ndani ya Bunge hili kuna Watanzania kwa mamilioni wa vyama na taasisi mbalimbali wanatisikiliza,” alisema.

Wakati wajumbe huyo anazungumza, baadhi ya wajumbe walipiga kelele na kuzomea hali iliyomlazimu kuacha kuzungumza na mwenyekiti kumsihi kuendelea, lakini Mbowe alisema: “Siwezi kuendelea wakati wajumbe wanapiga kelele.”

MAHALU

Mwenyekiti wa Kamati ya Kanuni na Kumshauri Mwenyekti wa Muda,Prof. Costa Mahalu, alisema kamati yake inapeleka mapendekezo kwa wajumbe na wenye maamuzi ni wajumbe na baadaye wanaagizwa kurekebisha mwafaka uliofikiwa na kuonyesha msimamo wao kwa pamoja.

Mjumbe wa Kamati, Bakari Khamis Bakari, alisema hakuna uhuru usiokuwa na kinga kulingana na maelezo ya maeneo husika na kwamba kamati italichukua suala hilo na kujadailiana ili kupata namna bora ya kuruhusu waandishi wa habari kuchukua habari.

George Simbachawene, mjumbe wa Kamati ya Kanuni na Kumshauri Mwenyekiti, alisema maoni ya kamati ni kuwa hisia na sababu wanazotoa wajumbe hao zilikuwapo kwenye kamati yao na walipenda waandishi waruhusiwe ili mchakato huo uonekane kwa umma wote.

“Kilichotushinda na kufikia uamuzi wa maoni hayo ni utekelezaji wake...kwa busara yetu tukaliwekea utaratibu kwenye fasili ya tatu, vyombo vyetu vya habari ni vingi, kamati iko ukumbi wa Msekwa asubuhi anakuja mwandishi anachukua anapeleka, habari zitakazokwenda juu ya hoja moja jambo moja zitakuwa hazijakamilika zitawachanganya wananchi na si kuwasaidia,” alisema.

Alisema waandishi watachukua habari kivyao na kuwachanganya wananchi na ndiyo maana wameamua mwenyekiti wa kamati atoe taarifa kwa waandishi.

DK. MWAKYEMBE
Dk. Harrison Mwakyembe alisema kitaaluma ni mwandishi wa habari na mwanasheria na kwamba anaona hakuna haja ya waandishi wa habari kuruhusiwa kuwepo kwenye kamati na badala yake wapewa taarifa na mwenyektii wa kamati husika.

Hata hivyo, baadhi ya watoa hoja, walipinga hatua hiyo huku wanaopinga waandishi kuingia kwenye ukumbi wakishangilia kwa kupiga meza kusisitiza waandishi kunyimwa kuingai kwenye kamati hizo, huku wachache wa vyama wa upinzani wakipinga uamuzi huo.

DK. TULIA ACKSON
Mjumbe wa Kamati ya Kanuni na Kumshauri mwenyekiti, Dk. Tulia Ackson, alisema hakuna uhuru usiokuwa na mipaka na kwamba kamati inapendekeza kifungu hicho kubaki jinsi kilivyo.

Hoja hiyo ilimalizika kwa wajumbe kupitisha kifungu jinsia kilivyo kuwa waandishi hawataruhusiwa kuingia kwenye kamati na badala yake watapewa taarifa na mwenyektii wa kamati.
CHANZO: NIPASHE