Kurasa

HARAKATI ZA MARAFIKI WA ELIMU NI NINI?

HARAKATI ZA MARAFIKI WA ELIMU NI NINI?
Ni harakati za watu wanaojali na wenye nia ya kuleta mabadiliko katika kuboresha elimu na demokrasia nchini. Harakati hizi zinawaleta pamoja wananchi wanaopenda maendeleo ya elimu na zinawapa fursa ya kubadilishana mawazo na uzoefu katika masuala yanayohusu elimu .Sera na mipango mbalimbali ikiwemo mpango wa maendeleo ya elimu ya msingi (MMEM) na mpango wa maendeleo ya elimu ya sekondari (MMES) inasisitiza ushiriki wa wananchi katika utekelezaji wake.Hivyo wananchi wote wanawajibu wa kuchangia uboreshaji wa elimu na demokrasia nchini. kujiunga na harakati hizi za marafiki wa elimu ni bure na hakuna malipo yoyote wasiliana nasi kwa namba 0755 65 00 75 au 0786 65 00 75 au e-mail jmrchrd@yahoo.com tukuunganishe na marafiki wa elimu popote ulipo Tanzania

Jumatano, 29 Januari 2014

serikali kusambaza tabuleti shule za sekondari nchini

Serikali inakusudia kutoa maelfu kwa maelfu ya tabuleti za kufundishia masomo mbalimbali kwa wanafunzi na walimu wa shule za sekondari nchini kama njia ya ubunifu zaidi, ya kisayansi na ya uhakika ya kukabiliana na changamoto zinazoikabili sekta ya elimu kwa kutumia Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (ICT).

Ili kufanikisha mpango huo, Serikali inakusudia kuingia ushirikiano na taasisi isiyokuwa ya kiserikali ya Opportunity Education Trust ya Marekani ambayo jana ilizindua mpango wa majaribio wa utoaji wa tabuleti hizo kwa wanafunzi na walimu wao wa shule za sekondari nchini.

Mpango wa Serikali wa kusambaza tabuleti kwa wanafunzi na walimu wa shule za sekondari ulitangazwa juzi na Rais Jakaya Kikwete, alipokutana na kuzungumza na Joe Ricketts, mwenye taasisi ya Opportunity Education Trust na mmoja wa matajiri wa Marekani.

Katika mazungumzo hayo yaliyofanyika Ikulu, Dar es Salaam, Rais Kikwete alimweleza kwa undani Ricketts hatua ambazo zimechukuliwa na Serikali yake kupania na kuboresha elimu tokea mwaka 2006, hatua ambazo zimechangia kupanua kwa kasi na kwa kiwango kikubwa wigo wa utoaji elimu nchini na changamoto ambazo zimezuka kutokana na upanuzi huo mkubwa.

Rais Kikwete alisema baadhi ya changamoto hizo ni ukosefu wa walimu na hasa wa masomo ya sayansi na ukosefu wa vitabu vya kufundishia, changamoto mbili kubwa ambazo zinatatuliwa na matumizi ya tabuleti.

“Mbali na upanuzi mkubwa wa nafasi za wanafunzi kupata elimu ya ngazi mbalimbali, pia tumepanua sana ufundishaji wa walimu. Mwaka 2005, vyuo vyetu vyote vilikuwa vinatoa walimu 500 sasa tunatoa walimu 12,000 kwa mwaka. Hivyo, tunaamini kuwa katika mwaka mmoja ama miwili ijayo, tutakuwa tumemaliza tatizo la walimu wa masomo ya sanaa,” alisema.

Hata hivyo, alisema bado nchi inakabiliwa na upungufu mkubwa wa walimu wa sayansi.

"Tuna upungufu wa walimu 26,000 na kwa mwaka vyuo vyetu vyote vinahitimisha walimu 2,100 tu," alisema.

Chini ya mpango huo wa majaribio wa kusambaza teknolojia hiyo ya kisasa, taasisi ya Opportunity Education Trust inatoa tabuleti 1,100 kwa ajili ya walimu na wanafunzi wa sekondari katika shule 33.

Ricketts alimwambia Rais Kikwete: “Hapa tunafanya majaribio na Tanzania ni nchi ya kwanza duniani miongoni mwa nchi ambazo tunaunga mkono mipango ya maendeleo kunufaika na mpango huo wa majaribio. Ni azma yetu kuwa baada ya kuwa tumefanya tathmini ya mafanikio na changamoto za hatua hii ya majaribio, tutaupanua mpango huu kushirikisha shule nyingi zaidi kwa kushirikiana na Serikali kwenye mpango wake mkubwa wa kusambaza teknolojia hii katika shule zote za sekondari hapa Tanzania.”

Ricketts na wataalam wake pamoja na maofisa wa Serikali walianza kutekeleza mpango huo jana kwa kutoa tabuleti kwa wanafunzi wa Shule ya Sekondari Wama Nakayama iliyoko mkoani Pwani.

Baada ya hapo, shughuli hiyo itahamia Zanzibar na Pemba, kabla ya Ricketts na wataalam wake kutoa tabuleti kwa shule zilizoko mikoa ya Arusha, Dar es Salaam, Dodoma, Mwanza, Kagera na Morogoro.

Shule zinazonufaika katika mpango huo ni za Serikali na binafsi na kwa kuanzia masomo ambayo yanapatikana katika tabuleti hizo ni Hesabu, Jiografia, Historia na Kiingereza.
 
chanzo ippmedia.com

Jumatatu, 27 Januari 2014

walimu wastaafu wa sayansi kupewa ajira tena

naibu waziri wa elimu philipo mulugo
Serikali imetangaza neema kwa walimu wastaafu wa somo la sayansi kujitokeza na kupeleka majina yao Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi ili waweze kupatiwa nafasi za kufundisha, kuziba pengo la ukosefu wa walimu hao nchini.

Hatua hiyo imechukuliwa ili kupunguza tatizo la upungufu wa walimu 26,000 uliopo hivi sasa hali inayoathiri zaidi wanafunzi wanaochukuwa masomo ya sayansi.

Hayo yalisemwa jijini Arusha na aliyekuwa Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philipo Mulugo siku moja kabla ya kuvuliwa wadhifa huo, wakati akizungumza katika mahafali ya tano ya chuo cha ufundi Arusha (ATC) ambapo jumla ya wanafunzo 256 walitunukiwa vyeti vya astashahada, stashahada na shahada ya kozi mbalimbali.

Alisema endapo walimu hao wastaafu hawatajitokeza, serikali itaingia hasara kubwa kutokana na kuajiri walimu wa fani hiyo kutoka nje ya nchi. Mulugo alisema serikali itawaombea kibali wizarani walimu wastaafu wa masomo ya sayansi watakaojitokeza  ili waweze kufundisha katika shule mbalimbali kwa kipindi cha miaka miwili na watakaopenda kuendelea hata kwa miaka 10 watakubaliwa.

“Tumekuwa tukitangaza sana kujitokeza kwa walimu wastaafu wa masomo ya sayansi nchi nzima kuleta majina yao wizarani ili waweze kupata ajira kwani tuna upungufu mkubwa sana, na tangu tutoe matangazo hayo wamejitokeza walimu wastaafu 96 tu, na hao hawatoshi bado tunawakaribisha sana popote pale walipo,” alisisitiza Mulugo.
 
Chanzo ippmedia.com

Jumamosi, 25 Januari 2014

Elimu bora; silaha ya kupambana na adui umaskini

Mwanahabari mkongwe, Othman Miraj anasema umaskini uliokithiri nchini ni suala lililogubikwa na mambo kadhaa yaliyosongamana.
Ni kwa sababu hiyo anasema ili kuumaliza umaskini, kunahitajika mipango na mikakati anuai, badala ya kuegemea katika kile anachosema dawa mujarabu ya aina moja.
“ Kuushinda umaskini ni kuwa na mkakati wa kuugawa utajiri wa Taifa, mifumo ya kisiasa duniani, kupigwa vita kwa ufisadi na kuwepo kwa mfumo mzuri wa elimu,’’ anataja baadhi ya mikakati ya kupambana na umaskini.
Mfumo bora wa elimu
Siyo Miraji tu, utafiti na uzoefu vinaonyesha elimu ni mojawapo ya silaha kubwa na muhimu siyo katika mapambano dhidi ya umaskini wa mtu mmojamoja, lakini pia katika maendeleo ya nchi kijamii na kiuchumi.
Wachambuzi wa sera na masuala ya kijamii, Elizabeth Missokia na Gervas Zombwe katika chapisho liitwalo ‘Hali ya Elimu Tanzania’, wanasema katika dunia ya leo, ili kila mtu aweze kuboresha maisha yake ni lazima awe na elimu.
Elimu ndiyo inayomwezesha mtu kujitambua na kujimiliki yeye mwenyewe, kuzikabili changamoto zinazomsonga, kuyatawala na kuyatumia mazingira yanayomzunguka ili kuboresha maisha yake
Wanaongeza kusema kuwa ndani ya utandawazi, elimu isiyotosheleza, tafsiri yake ni umaskini zaidi; wakati elimu zaidi tafsiri yake ni maisha bora zaidi.
Ili elimu iweze kuleta mabadiliko ya kweli kimaendeleo ni lazima iwe elimu bora, ambayo inalenga kumbadilisha mtu na kumwezesha kufikiri, kubuni, kujitambua, kuhoji, kudadisi, kupenda kazi, kuwa na mwenendo mwema na kuboresha afya na maisha yake binafsi na ya jamii, wanaongeza kusema.
Umuhimu wa elimu hasa kwa mabadiliko ya mtu binafsi kuelekea mafanikio ya kijamii,unadhihiri pia katika kauli maarufu ya aliyekuwa Rais wa kwanza mzalendo wa Afrika Kusini, Nelson Mandela aliyesema:
“........elimu ni injini kubwa ya maendeleo ya mtu. Ni kupitia elimu ndipo binti wa mkulima mdogo anaweza kuwa daktari bingwa, kwamba mtoto wa kibarua wa mgodini anakuwa mkuu wa mgodi na mtoto wa kibarua wa mashambani anakuwa Rais wa Taifa kubwa”.
Elimu bora ni ipi?
Kwa kawaida, mfumo wa elimu bora huzaa elimu bora na hii ndiyo aina ya elimu tunayoitaka Tanzania kwa maendeleo ya kiuchumi na ustawi wa wananchi wake.
Swali kuu ni; elimu bora ni ipi? Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk Ahmed Kiwanuka anasema elimu bora ni ile inayomkomboa binadamu na kumwezesha kuchangia katika jamii na taifa kwa kazi atakazokuwa akizifanya.
“Lengo la kupata elimu ni kumkomboa mtu kutokana na utumwa wa umaskini. Inatakiwa elimu imwezeshe mtu kutumia fikra zake kuendesha maisha mara baada ya kuhitimu masomo yake,” anasema
Akirejea maneno ya Mwalimu Julius Nyerere, anasema mwanafalsafa huyo aliyekuwa mtetezi mkubwa wa elimu aliwahi kusema kuwa ukombozi wa watu maskini utatokana na kusoma.
“Ukimwelimisha mtoto wa masikini, utakuwa umeisaidia familia yake, jamii na hata Taifa kutokana na mchango atakaotoa baada ya kuelimika,” anaeleza Dk Kiwanuka na kuongeza:
“Wasomi wetu wanatakiwa kujitoa kwa jamii kuhakikisha wanatumia elimu walioipata kwa ajili ya wengine.Taifa lolote linalotaka kuendelea lazima liwekeza zaidi katika elimu kwa kuwasomesha watu wote bila kuwabagua.”
Naye Rais wa Chama Cha Walimu Tanzania (CWT), Gratian Mukoba, anasema elimu bora ni ile inayozingatia mambo muhimu matatu, ambayo ni maarifa, ujuzi na mtazamo.
“Ukiwa na mambo hayo mwanafunzi atakuwa anajitambua na ataelewa maisha ni kitu gani. Ndivyo vitu vitakavyomwezesha kujua namna ya kuitumia elimu katika maisha ya kawaida katika jamii inayomzunguka,” anasema Mukoba.
Vikwazo vya elimu bora 
Licha ya kuwepo kwa juhudi kadhaa zinazofanywa na Serikali na wadau wengine wa elimu zinazolenga kuimarisha elimu nchini, bado sekta ya elimu inakabiliwa na vizingiti kadhaa vinavyohatarisha utoaji wa elimu na hata mustakabali wa sekta kwa jumla.
Tafiti na uzoefu vinaonyesha vikwazo vikubwa vya elimu nchini ni pamoja na taifa kukosa dira maalumu kuhusu elimu na aina ya mafunzo au maarifa, ambayo wanafunzi wanapaswa kufundishwa au kujifunza kutegemea mahitaji ya wakati uliopo.
Dira ni mwongozo wenye malengo yanayolinda utoaji wa elimu kwa manufaa ya nchi na mtu binafsi.


Changamoto nyingine zinazotajwa na wataalamu wa elimu kupitia utafiti wao ni kasoro za mitalaa, ikiwamo baadhi yake kuwa na masomo yasiyotoa ujuzi wa maana kwa wahitimu, hivyo kushindwa kukabiliana na changamoto za kimaisha.
Nyingine ni kuendelea kutumia lugha ya Kiingereza katika kufundishia shule za msingi, ambayo haifahamiki kwa wanafunzi na walimu wenyewe, uhaba wa walimu hasa katika masomo ya sayansi na hesabu, uwepo wa walimu wenye uwezo mdogo kitaaluma na kufundisha, uhaba wa vifaa vya kufundishia na kujifunzia na baadhi ya wanajamii kutojali elimu kwa watoto wao.

chanzo mwananchi

Mapenzi ya jinsia moja yalalamikiwa sekondari wasichana

Shule moja ya sekondari ya wasichana iliyopo wilayani Bagamoyo mkoani Pwani,  imelalamikiwa na wanafunzi pamoja na wazazi kuwa mabinti wanajihusisha na vitendo vya ngono vya jinsia moja (usagaji).

Akizungumza na NIPASHE mmoja wa wazazi (jina linahifadhiwa)  alisema shule hiyo imepoteza sifa kwa kuwa kuna wimbi kubwa la wanafunzi wanaojihusisha na vitendo hivyo vya usagaji.

Alisema  mtoto wake alikuwa ameanza kidato cha kwanza mwaka jana na baada ya kumuandikisha ndipo baadhi ya watu walipomueleza kuwa shule hiyo kwa sasa ina sifa mbaya ya mchezo ‘huo mchafu.’

"Baada ya kuelezwa nikasema nitalifanyia kazi jambo hilo hivi karibuni katika kupekua madaftari ya mwanangu nakutana na kibarua cha mapenzi alichoandikiwa na msichana mwenzake niliumia sana na nilitumia nguvu kumbana bila hivyo asingeniambia," alisema

Alisema ilimbidi amhamishe binti yake na kujiunga na shule moja ya sekondari iliyopo mkoani Tanga kwa ajili ya kuendelea na masomo ya kidato cha pili mwaka huu.

Mzazi huyo alisema anashangazwa ni kwa nini hatua hazichukuliwi wakati suala hilo ni la hatari kwani watoto wao wataharibika kiakili pamoja na kimwili na wanaweza kuambukizana VVU na Ukimwi..

Alisema wakati mwanaye akisoma katika shule hiyo alikuwa akihudhuria vikao vya wazazi mara kwa mara na kwamba kila kikao walikuwa wakifukuzwa wanafunzi kutokana na mwenendo huo.

"Hili tatizo ni kubwa na kufukuzwa kwa mwanafunzi sidhani kuwa wanatatua tatizo nadhani hakuna usimamizi mzuri kwani wangeweza kudhibiti kwa haraka tatizo hilo kabla ya kuwa kubwa," alisema

Pia alisema ndugu yake imembidi amhamishe mwanae na kumtafutia shule nyingine kwa kuhofia binti yake  kurubuniwa kwani wanakuwa ni wadogo na hawaelewi chochote, hivyo inaweza kuwa rahisi kudanganywa na kuingia kwenye vitendo hivyo viovu.

Alisema kuwa hata kiwango cha ufaulu kwa sasa shule hiyo imeshuka kutokana na tatizo hilo kwa wanafunzi .

Hata hivyo, NIPASHE  ilizungumza na mwanafunzi mmoja ambaye anasoma katika shule hiyo kuhusiana na suala hilo ambapo alikiri kuwepo kwa jambo hilo na kueleza kuwa wanaofanya mchezo huo ni wa kidato cha tano na cha sita.

"Mimi hawajanifanyia ila najua wanaofanya mchezo huo ni wale walioko kidato cha tano na cha sita," alisema Pia kuna baadhi ya wazazi wengine wamekuwa wakilalamikia jambo hilo na kueleza kuwa ndugu zao imewalazimu kuwahamisha watoto wao kutokana na vitendo hivyo vinavyofanyika shuleni hapo.

CHANZO: NIPASHE

Jumatano, 22 Januari 2014

mabadiliko baraza la mawaziri kila mmoja na mtizamo wake

Hatimaye Baraza jipya la Mawaziri limetangazwa , tumeshuhudia mabadiliko katika Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi ambapo Naibu Waziri wa Elimu wa sasa ni Mh. Jenista Mhagama amechukua nafasi ya Mh. Philipo Mulugo. Wako watanzania wanayaona mabadiliko haya kutokuwa na tija huku wengine wakiamini mabadiliko yanaweza kutokea, wote wana sababu za msingi kabisa kuamini kile wanachoamini. Je mdau wa elimu ni mambo yapi Uongozi wa sasa unatakiwa kuyazingatia/kuyafanya ili kuhakikisha kiwango cha elimu nchini kinapanda na wanafunzi kote nchini wanapata elimu bora? Tafakari na tushikirikishane
 
chanzo haki elimu facebook page

Habari TATU KALI zinazohusu masuala ya Elimu nchini Tanzania zinazopamba katika vyombo vya habari tarehe 22 January 2014



1. Wanafunzi 11,000 katika mkoa wa DSM wamekosa nafasi za kujiunga na kidato cha kwanza licha ya kufaulu mtihani wa darasa la saba mwaka jana. (Chanzo: Habari Leo)

2. Mkuu wa Wilaya ya Nzega ameagiza wanafunzi wote wa shule za msingi na sekondari wilayani humo waliokatishwa masomo yao kwa sababu mbalimbali ikiwemo mimba, utoro n.k (Chanzo:Tanzania Daima)

3. VETA yaanzisha maabara za LUGHA katika vyuo vyake ili kuwezesha ufundishaji wa lugha za kigeni kwa ubora zaidi na kuondoa tatizo la watanzania kushindwa kujieleza kwa lugha za kigeni. ( Chanzo: The Guardian)
 
chanzo haki elimu page

Jumanne, 21 Januari 2014

waliofeli kidato cha pili kuendelea na masomo

Wakati Watanzania wakisubiri matokeo ya kidato cha pili mwaka 2013, imebaini kuwa Serikali imetoa agizo kwamba wanafunzi wote waliofeli mtihani huo kuendelea na masomo ya kidato cha tatu, huku wakisoma mafunzo ya kurudia mtihani wa kidato cha pili.

Licha ya matokeo hayo kutotangazwa hadi sasa, imebainika kuwa waliofaulu mtihani huo uliofanywa Oktoba 7 hadi 21 mwaka jana ni asilimia 62 tu, asilimia 31 wakitakiwa kukariri (kurudia) kidato cha pili mwaka huu, huku asilimia saba wakishindwa mtihani huo kwa mara ya pili.

Jumla ya wanafunzi 531,457 walitajwa na Wizara ya Elimu mwaka jana kuwa watafanya mtihani huo.

Uamuzi huo wa Serikali ni tofauti na ule uliotolewa na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk Shukuru Kawambwa Novemba 4, mwaka 2012, kwamba kuanzia wakati huo mtihani wa kidato cha pili utakuwa ni wa mchujo na kwamba atakayefeli atatimuliwa.

Dk Kawambwa alisema matokeo ya mtihani wa kidato cha pili yatatumika kama kigezo cha kuchuja na kukariri kidato cha pili kwa watahiniwa watakaoshindwa kufikia wastani wa ufaulu wa alama 30.

Alisema mtahiniwa ataruhusiwa kukariri kidato cha pili mara moja tu na endapo mtahiniwa atashindwa mtihani kwa mara ya pili kwa mwaka utakaofuatia, itabidi aendelee na elimu ya sekondari nje ya mfumo rasmi.

Gazeti hili limeiona barua iliyoandikwa Januari 16 mwaka huu na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi na kusainiwa na Katibu Mkuu wake, Profesa Sifuni Mchome, kwenda kwa wadau wa elimu nchini, wakiwamo maofisa elimu wa mikoa na Chama cha Wamiliki wa Vyuo na Shule Binafsi (TAMONGSCO).

Katika barua hiyo, wizara hiyo imewataka wadau hao kuhakikisha kuwa wanafunzi watakaofeli mtihani huo, wanaendelea na masomo ya kidato cha tatu.

“Matokeo ya kidato cha pili yamepokewa na kufanyiwa uchambuzi ili kupata taswira ya taifa. Taarifa ya matokeo hayo imebaini kuwa watahiniwa waliofanya mtihani na kufaulu ni sawa na asilimia 62 tu,” inaeleza sehemu ya barua hiyo na kuongeza;

“Hali hii inaonyesha kuwa asilimia 31 ya wanafunzi watatakiwa kukariri kidato cha pili, 2014. Wale walioshindwa kwa mara ya pili ambao ni asilimia saba wanatakiwa kuendelea na masomo nje ya mfumo rasmi.”

Barua hiyo inaeleza kuwa wanafunzi waliofaulu kwa wastani wa alama 20 na kuendelea waendelee na masomo ya kidato cha tatu mwaka 2014, wakati awali Serikali ilitoa tamko kuwa watakaoshindwa kufikisha alama 30 watatimuliwa.

“Wanafunzi waliofaulu kwa wastani wa alama 20 hadi 39 wapewe mafunzo rekebishi ‘Remedial class’ wakiwa kidato cha tatu,” inaeleza sehemu ya barua hiyo.


Inaeleza kuwa uamuzi huo unawahusu wote wakiwamo wale walioshindwa kwa mara ya pili, “Kwa maana hiyo hakuna mwanafunzi atakayerudishwa nyumbani.”

Mwisho barua hiyo imewataka wadau hao kuhakikisha kuwa inawapa taarifa mameneja na wamiliki wa shule na seminari ili kusimamia utekelezaji wa uamuzi kuhusu matokeo hayo.

Kauli ya wizara

Akitolea ufafanuzi suala hilo, Profesa Mchome alisema, “Suala la wizara kuagiza wanafunzi wote waliofeli kuendelea na masomo ya kidato cha tatu mimi sijalisikia, ninachojua ni kwamba wapo watakaorudia.”

Alisema kuwa tayari wizara imeshapeleka taarifa za matokeo hayo na uamuzi wa Serikali katika kila kanda nchini. “Kila shule ina taarifa hizo. Wapo wanafunzi watakaorudia.”

Akizungumza kuhusu matokeo ya kidato cha pili mwaka 2013 kutotoka mpaka sasa alisema, “Ninachofahamu ni kwamba matokeo ya kidato cha pili yameshawasilishwa katika kanda zote nchini.”

“Unajua matokeo ya kidato cha pili siyo kama matokeo ya darasa la saba, kidato cha nne na sita. Matokeo ya kidato cha pili ni kama mwendelezo wa tathmini ‘Continuous assessment’ kwa mwanafunzi, hutumika pia katika mtihani wa kidato cha nne.”

Alisema ndiyo maana matokeo hayo hupelekwa katika shule husika. “Baada ya kupelekwa katika shule husika, hapo ndipo inaweza kutolewa taarifa za matokeo hayo pamoja na ufafanuzi.”

Kwa nyakati tofauti gazeti hili lilimtafuta Dk Kawambwa na Naibu wake, Phillip Mulugo ili kutolea ufafanuzi suala hilo, lakini simu zao za mkononi zilikuwa zikiita bila majibu.

Msimamo wa TAMONGSCO

Alipotafutwa Katibu Mkuu wa Tamongsco, Benjamin Nkonya kueleza kama wanakubaliana na agizo hilo la Serikali alisema, “Inaonekana Serikali haiko tayari kutekeleza mkakati wake wa Matokeo Makubwa Sasa (BRN).”

“Kama wizara inalazimisha wanafunzi walio na ufaulu mdogo kuendelea na masomo katika mfumo wa vidato (formal education), lazima tutegemee kuona wanafunzi wakifanya vibaya katika mitihani ya kidato cha nne.”

Alisema kuwa asilimia 98 ya wanachama wa chama hicho ni Watanzania wazalendo kwamba hawapo tayari kutekeleza agizo la Serikali kwa sababu siyo la kizalendo na limetolewa kwa ajili ya kutimiza malengo ya kisiasa ya kujiongezea umaarufu wa muda mfupi, huku Watanzania wakiogelea kwenye dimbwi la umaskini unaotokana na ujinga.

“Wachache watakaosaliti msimamo huu watakuwa wamekubali kupoteza muda wa vijana wetu huku wakijua kwamba watafika kidato cha nne, kupata daraja sifuri na kuishia kuwa machangudoa, wauza dawa za kulevya, bangi, wizi na vitendo vingine vya uvunjifu wa sheria, kanuni na taratibu,” alisema.

Alisema ili kuwasaidia wanafunzi wanaoshindwa kuendelea na masomo yao; “Mwanafunzi ambaye ufaulu wake utakuwa chini ya asilimia 45 aondolewe katika mfumo wa elimu ya vidato (formal education) na kuingizwa katika mfumo wa elimu ya ufundi mchundo (TVET - Technical education and vocational education).”

Alisema wanachama wa Tamongsco wanamiliki vyuo 586 kati ya vyuo 750 vya ufundi mchundo (VETA) na wanamiliki vyuo 1975 kati ya vyuo 1988 vya ufundi stadi (technical institutes) ambavyo vinasimamiwa na Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi Stadi (NACTE).

“Vyuo hivi vina uwezo wa kuchukua wanafunzi wote ambao wana ufaulu wa chini ya asilimia 45 kuwaendeleza hadi chuo kikuu. Kikwazo pekee kilichopo ni kwa Serikali kukubali kuchangia gharama za uendeshaji wake.”

“Kikwazo hiki kitaondoka endapo Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi itakubali kutekeleza sera, sheria na kanuni za ushirikiano kati ya sekta ya umma na binafsi (PPP) partnership) kama ilivyopitishwa na Bunge mwaka 2010.

Kidato cha pili 2012

Katika mtihani huo mwaka 2012 wanafunzi 136,923 kati ya 386,271 waliofanya mtihani huo walifeli. Idadi ya waliofeli ilikuwa sawa na asilimia 35.5, wakiwamo wasichana 74,020 na wavulana 62,903, waliofaulu walikuwa wanafunzi 245.9,32.


CHANZO: Mwananchi

Ijumaa, 10 Januari 2014

Baba wa miaka 54 aoa mtoto wa miaka minane

Bunda. Polisi Wilaya ya Bunda, wanamshikilia baba mwenye umri wa miaka 54 kwa tuhuma kuoa mwanafunzi wa kike wa umri wa miaka minane.
Msimamizi wa Dawati la Jinsia katika Kituo Kikuu cha Polisi Bunda, Rita Charles alisema baba huyo mkazi wa Kijiji cha Nyaburundu wilayani Bunda alikamatwa jana akiwa anaishi na binti huyo (jina limehifadhiwa) kama mke wa nyumbani baada ya kutoa kishika uchumba kiasi cha Sh55,000 kwa wazazi wake.
Ilielezwa kuwa mwanaume huyo kabla ya kumwoa mtoto huyo aliyekuwa anasoma darasa la kwanza katika Shule ya Msingi Nyaburundu, alimchumbia kwa wazazi wake na kutakiwa atoe ng’ombe watano za mahari ndipo akatoa kishika uchumba hicho na mtoto huyo kuondolewa shule. “Tulifanikiwa kumkamata mwanamume huyo baada ya kupata taarifa kutoka kwa wasamaria wema,” alisema Rita.
Alisema siku ya Mwaka Mpya, alichukuliwa na dada yake na kumpeleka kwa mume wake huyo ili aanze maisha ya ndoa.
Hata hivyo, alisema alipofika, usiku huo walilala kitanda kimoja wote watatu (baba muoaji, muolewaji na dada wa muolewaji) na kwamba mwanamume huyo alianza kufanya mapenzi na dada yake na baadaye akamgeukia ‘mkewe’ kuanza kumnyonya maziwa.
“Tulilala wote watatu na alifanya mapenzi na dada yangu, mimi akininyonya maziwa,” alisema mtoto.

chanzo. mwananchi

uandikishwaji wa wanafunzi darasa la kwanza baadhi ya mikoa kuna changamoto

Zoezi la uandikishaji wa wanafunzi wapya wa darasa la kwanza mwaka huu limeanza na misukosuko ya aina yake. Baadhi ya maeneo nchini yamekumbwa na mgogoro mkubwa baina ya wazazi na walimu, chanzo kikitajwa kuwa ni pamoja na gharama ambazo kila mtoto hutakiwa alipiwe na wazazi wake kabla ya kupatiwa fursa ya kuandikishwa.

Taarifa zilizoripotiwa jana zilionyesha kuwa mjini Morogoro hali haikuwa shwari. Vurugu kubwa ziliibuka na mwishowe baadhi ya wazazi wanaodaiwa kuwa ni wenye itikadi tofauti za vyama walivaana mwilini.

Katika kisa hicho, inalezwa kuwa kila mzazi alitakiwa alipe walau Sh.50,000 ndipo kila mtoto aliyempeleka shuleni apate fursa ya kuandikishwa. Kwamba, baadhi ya wazazi wenye uwezo kifedha walilipia gharama hizo bila shida. Hata hivyo, wengine wakataka watoto wao waendelee kuandikishwa hata kama walikosa fedha hizo kwavile si sera ya serikali kuwabagua wananchi wake kwa kigezo cha pesa.

Inadaiwa kuwa sintofahamu hiyo ikakolezwa na itikadi za vyama baada ya mzazi mmojawapo anayedaiwa kuwa ni wa chama tawala kutetea ulipaji wa gharama hizo huku mwingine anayedhaniwa kuwa ni wa upinzani akipinga vikali. Mwishowe wawili hao wakavaana kwa nia ya kushikishana adabu. Walishindwa kukubaliana juu ya kutofautiana kwao.

NIPASHE hatukusudii kujadili ugomvi baina ya wazazi hao wa Morogoro. Na wala siyo lengo letu pia kuwa mahakimu na kueleza ni nani kati yao aliye sahihi. Bali, tunalichukulia tukio hili kuwa ni mfano wa kile kinachotokea katika maeneo mengi nchini.

Kwamba, katika kipindi hiki, baadhi ya walimu wakuu huwageuza wazazi kuwa mtaji. Huanzisha michango mingi kwa visingizio mbalimbali, lengo likiwa ni kuwakamua wazazi hadi tone la mwisho. Katika hili, sisi hatuoni kuwa ni sahihi. Siyo haki hata kidogo kuwabebesha wazazi mzigo mzito wa gharama za elimu kupitia rundo la michango inayoanzishwa kwa visingizio mbalimbali.

Kwa mfano, sisi tunaona kuwa kuwalazimisha wazazi kulipa Sh. 50,000 kwa kila mtoto ndipo haki ya kuandikishwa shule ipatikane siyo uamuzi sahihi. Tunaamini hivyo kutokana na ukweli kuwa mara zote, serikali yetu imekuwa ikisisitiza kuwa elimu ya msingi ni lazima kwa kila mtoto aliyefikisha umri wa kwenda shule. Tena, kadri ya ufahamu wetu, elimu hii hutolewa bure.

Abadan, michango ya aina yoyote ile haiwezi kuwa chanzo cha mwanafunzi wa darasa la kwanza kunyimwa haki yake ya kuandikishwa. Na ndiyo maana, kwa tukio la Morogoro, Mbunge wa Jimbo hilo aliingilia kati na kuwataka walimu kuwaandikisha watoto wote bila kujali kama wazazi wao wamelipa mchango wa Sh. 50,000 ama la. Ni kwa sababu elimu ya msingi ni ya lazima, na tena ni haki ya kila mtoto.

Isitoshe, kwa mujibu wa nyaraka mbalimbali za elimu nchini, umri wa kuanza darasa la kwanza una ukomo wake. Kutomuandikisha mtoto aliyefikia umri wa kuanza shule ni kumpa adhabu asiyostahili kwani kuna uwezekano mkubwa wa kukataliwa katika mwaka unaofuata kutokana na kigezo cha kuwa na umri mkubwa. Matokeo yake, taifa litakuwa katika hatari ya kuwa na idadi kubwa ya watu wasiojua kusoma na kuandika. Hili siyo jambo zuri hata kidogo.

NIPASHE hatupingi hatua ya wananchi kutakiwa kuchangia maendeleo yao, yakiwamo ya elimu. Hata hivyo, michango hii haipaswi kuwa chanzo cha kuongeza kwa idadi ya wasiojua kusoma na kuandika. Haipaswi vilevile kuwa chanzo cha kuligawa taifa kwa misingi ya wenye nacho na wasio nacho. Isitoshe, tunadhani kwamba sasa kuna kila sababu kwa viongozi wanaosimamia elimu kuingilia kati na kusimamia kwa vitendo kauli zao mbalimbali zinazosisitiza kuwa elimu ya msingi ni ya lazima kwa kila mtoto na kwamba, hakuna ada wala michango yoyote ya lazima.

Kuachia hali iendelee kuwa kama Morogoro ni hatari. Ni kuichafua serikali ambayo lengo lake zuri la kutoa elimu ya msingi bure linaelekea kutibuliwa na watu wachache walio na vipaji vya kubuni kila aina ya michango ili kuwakamua wazazi kwa maslahi yanayotiliwa shaka.

Michango mingi kama ya madawati, ya uji, ya ulinzi, ya nembo za shule na ya mitihani kwa shule za msingi haipaswi hata kidogo kutumiwa kwa maslahi ya wachache kwani athari za kuwa na taifa lililojaa watu wasiojua kusoma na kuandika ni kubwa sana na kamwe hazipimiki kirahisi.

Shime, michango hii katika uandikishaji wa wanafunzi wapya wa darasa la kwanza isitumiwe kubagua wasio na uwezo.

chanzo Nipashe